2013-06-14 07:27:08

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 11 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa


Ni kama kawaida tunakutana tena katika viunga vya Radio Vatican kushirikishana pendo la Mwenyezi Mungu kwa njia ya Neno lake. Ni Dominika ya 11 katika kipindi cha kawaida cha mwaka C. Mama Kanisa atufundisha Neno la Mungu lenye kuokoa na kuleta msamaha. RealAudioMP3

Tunasikia katika somo la kwanza maneno ya faraja toka kwa Mungu kupitia kinywa cha Nathani akimwelekea Daudi mdhambi “Bwana naye ameiondoa dhambi yako hutakufa” Katika Injili Bwana mwenyewe Nafsi ya Pili ya Mungu anamwambia mwanamke mkosefu “Imani yako imekuokoa enenda zako kwa amani”. Basi tokea katika upendo huu ulio mkamilifu Mt Paulo anasema kwa hakika lazima asulubiwe katika Kristo na Kristo awe hai ndani yake.

Mpendwa msikilizaji, ujumbe wa Neno la Mungu ni kuishi unyenyekevu na kuomba msamaha vinavyotuletea heri na baraka tele katika maisha yetu. Mfalme Daudi katika somo la kwanza anaonekana kupokea msamaha si kwa sababu ya jambo jingine zaidi ya kutamka mbele ya mtumishi wa Mungu baada ya kutangaziwa uovu wake akisema: “nimekosa mbele ya Mungu” na mara moja baada ya kusema maneno haya ya toba anapata ondoleo la dhambi. Tendo hili la Mfalme Daudi latukumbusha pia mfano wa mwana mpotevu, anapoona maji yako shingoni kimbilio lake ni kuomba msamaha na mara moja anafanyiwa sherehe kubwa pasipo kutarajia.

Mama amabaye ambaye tumemsikia katika Injili katika mazingira yale alikuwa kahaba na hivi jumuiya ilimwona kama kinyaa na kama mtu asiyestahili kumgusa Masiha. Katika udhaifu wa huyu mama na unyenyekevu wa Mungu kunazaliwa msamaha ambao haukutarajiwa machoni pa Mafarisayo au tuseme walinda sheria. Mama huyu anapomgusa Bwana, mara moja tunaona anaingia katika safari ya toba inayoambatana na tumaini katika Bwana aliye mkombozi wake. Mama huyu anapokea furaha ya Yesu mfufuka na anaambiwa imani yako imekuponya.

Gharama ya msamaha ni imani na kweli imani inaokoa. Mpendwa msikilizaji mara nyingi katika maisha yetu tunapenda kulipiza na kuadhibu wakosefu na hata kuwatupilia mbali toka mazingira yetu, lakini leo Bwana anawaleta karibu watoto wake waliowakosefu wakakae karibu naye. Anathibitisha kuwa kile alichokitangaza aliposoma chuo cha Nabii Isaya ni kweli katika maisha yake. Nimekuja kwa ajili ya walio maskini (Lk. 4:18).

Basi mpendwa msikilizaji itikieni wito wa Bwana, mwalikeni maishani mwako kama Mt. Paulo asemavyo kwangu mimi kuishi ni Kristu, nimesulibiwa katika yeye na maisha yangu yanaendana na wito wa Mungu wa kutangaza mapendo kwa wadhambi na wema.

Nikutakieni mapendo na jicho la msamaha katika utumishi na maisha yako yote.
Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.