2013-06-14 14:38:41

Makanisa yaendeleze matunda ya majadiliano ya kiekumene kwa kuonesha Mshikamano wa Kiimani katika Sala na Uinjilishaji


Askofu mkuu Justin Welby wa Jimbo kuu la Cantebury na kiongozi mkuu wa Kanisa Anglikani amewashukuru viongozi wa Kanisa Katoliki ambao kwa takribani kipindi cha miaka hamsini iliyopita wameonesha namna na jinsi ya kugusa mioyo ya watu kwa njia ya mshikamano wa upendo, changamoto kwa Wakristo kuchuchumilia umoja miongoni mwao na kwa vile upendo unaonesha hali tofauti kabisa.

Askofu mkuu Welby anakiri kwamba, ndani mwake anabeba utajiri mkubwa wa Mafundisho Jamii ya Kanisa na Tafakari mbali mbali ambazo amebahatika kuzipata katika hija ya maisha yake kiasi kwamba, hija yake mjini Vatican inamfanya kujisikia kuwa yuko nyumbani. Wakristo wanaalikwa kuchuchumilia umoja na udugu miongoni mwao ili kuendeleza mchakato ulioanzishwa na viongozi wa Makanisa haya mawili katika kipindi cha miaka hamsini iliyopita. Ni matumaini yake kwamba, viongozi hawa wawili watasaidia jitihada za upatanisho kwa ulimwengu na Kanisa.

Wanapaswa kuendeleza matunda ya majadiliano miongoni mwa Maaskofu, kwa kuonesha mshikamano wa imani katika sala na Uinjilishaji.Ushuhuda wa umoja na mshikamano utasaidia kukoleza misingi ya amani na upatanisho, ingawa bado wanakabiliwa na changamoto mbali mbali. Jambo la msingi ni kujiaminisha kwa Kristo na kwamba, urafiki uliojionesha miongoni mwao utawasaidia kujenga umoja, kushirikishana mang'amuzi na kusaidia kubeba majukumu yao, daima wakiwa waaminifu kwa utashi wa Kristo kwa wafuasi wake.

Upendo wa Kristo uwasaidie kuibeba vyema Misalaba yao na kujifisha, ili kutoa nafasi kwa Kristo aweze kuishi ndani mwao, kwa kuonesha ukarimu na upendo kwa maskini. Ni changamoto ya kushikamana ili kukabiliana na vita na madhulumu dhidi ya Wakristo sehemu mbali mbali za dunia; kusimama kidete dhidi ya Serikali zisizozingatia utawala bora na haki uchumi, kwani wao kama viongozi ni sauti ya kinabii.







All the contents on this site are copyrighted ©.