2013-06-14 14:50:43

Kukiri dhambi ni kielelezo cha unyenyekevu na unyofu wa moyo!


Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kutambua ubinadamu na unyonge wao unaoweza kuwatumbukiza katika dhambi, ili wawe tayari kupiga moyo konde na kumwendea Yesu Kristo huku wakiungama dhambi zao kama alivyofanya Mtakatifu Paulo katika hija ya maisha yake ya imani.

Kuungamana dhambi ni kielelezo cha unyofu na moyo wa unyenyekevu unaopaswa kuoneshwa kwa namna ya pekee na Makleri, waliopewa dhamana ya kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, wao kama viongozi wa Kanisa wamepewa wito na dhamana hii katika chombo cha udongo kama yasemavyo Maandiko Matakatifu.

Msalaba wa Kristo uwe ni kielelezo cha changamoto ya maisha na utume wao kwa Kristo na Kanisa lake. Kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wa Kristo, mwanadamu amekirimiwa ukombozi kutoka kwa Kristo. Kila mwamini anayekutana na Yesu kwa kutambua udhaifu wake, anakirimiwa neema ya utakaso na mageuzi makubwa kama ilivyotokea kwa yule Mwanamke Msamaria na wafuasi wengine wa Yesu.

Baba Mtakatifu Francisko ameyasema hayo Ijumaa, tarehe 14 Juni 2013, wakati wa Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Mathae kilichoko mjini Vatican. Ibada hii imehudhuriwa na Viongozi wakuu na wafanyakazi wa Baraza la Kipapa la Makleri.







All the contents on this site are copyrighted ©.