2013-06-14 14:48:33

Jikiteni zaidi katika: majadiliano, utambuzi na daima muwe mstari wa mbele kutekeleza wito na utume wenu katika ulimwengu wa utamaduni!


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 14 Juni 2013 amekutana na Jumuiya ya Waandishi wa Jarida la "Civiltà Cattolica" na kuwashukuru kwa mchango, ushirikiano na mshikamano na Khalifa wa Mtakatifu Petro tangu mwaka 1850 na kuwataka kuendeleza utume wao kwa kuzingatia mambo makuu matatu: majadiliano; utambuzi na daima kuwa mstari wa mbele wanapotekeleza utume wao.
Baba Mtakatifu anasema Jarida hili linatoa mchango mkubwa katika majiundo ya watu na kwamba, katika kipindi cha miaka 163 tangu lilipotolewa kwa mara ya kwanza limepitia mabadiliko makubwa kwa kusoma alama za nyakati. Wanapaswa kuendelea kuwa waaminifu kwa Kanisa ili kupambana na ukakasi wa mioyo na unafiki unaotokana na baadhi ya watu kutaka kujifungia katika ubinafsi, dalili za ugonjwa.

Wao wawe ni madaraja ya majadiliano kati ya waamini na wasioamini ili kutafuta ukweli ambao kimsingi ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa kutajirishana, kushirikishana na kujinyenyekeza kama sehemu ya mchango wa majiundo endelevu na mafao ya wengi.

Jumuiya hii ijitahidi kuzima kiu ya wasomaji wake kwa njia ya mwanga wa Injili kwa kujibu maswali msingi yanayowatatiza watu wengi kwa nyakati hizi; wawasaidie watu kumwona Mungu katika maisha na tamaduni zao; Mungu ambaye anaendelea kufanya kazi kwa njia ya Roho Mtakatifu katika uhalisia wa medani mbali mbali za maisha ya mwanadamu.

Kama waandishi wa Jarida hili watoe kipaumbele cha pekee katika ukweli, wema na uzuri wa Mwenyezi Mungu; wasimame kidete kulinda na kutetea maisha ya binadamu na utunzaji bora wa mazingira, kamwe wasipatwe na kishawishi cha kujitafuta wenyewe, kwani wataugua na kuzeeka vibaya, changamoto kwao na kwa Kanisa kuendelea kuwa na ari na moyo wa ujana.

Baba Mtakatifu anawaalika waandishi hao kuwa mstari wa mbele katika ulimwengu wa utamaduni kwa kuonesha umahiri na mwono halisi wa imani ya Kikristo, ili Injili iweze kumwilishwa katika uhalisia wa maisha ya watu, kwani, huu ndio utume halisi wa Wayesuit kuvuka vikwazo na vizingiti ili kuwashirikisha watu Injili ya Kristo. Wawe ni watu walioko mstari wa mbele.

Anawapongeza kwa mabadiliko makubwa waliyoyafanya kwenye Jarida hili kwa mwaka huu, kiasi kwamba, linaweza kusomwa hata kwenye mtandao na watumiaji wa mitandao ya kijamii. Huu ni mwelekeo mzuri unaopaswa kuendelezwa. Jarida hili linapata chimbuko lake katika maisha na majiundo ya watu, kila mtu anapaswa kuchangia kadiri ya uwezo na karama zake na kwamba, anawategemea katika utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.







All the contents on this site are copyrighted ©.