2013-06-14 08:03:38

Injili ya Uhai na changamoto zake ulimwenguni


Maadhimisho ya Kilele cha Siku ya Injili ya Uhai Jumapili, tarehe 16 Juni 2013 sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani ni tukio maalum linalopania kuonesha mwanga wa Injili dhidi ya utamaduni wa kifo unaojionesha katika masuala ya kifo laini, utoaji mimba na matumizi ya viinitete katika majaribio ya kimaabara.

Ni tukio ambalo Mama Kanisa anapenda kulitumia kwa ajili ya kutangaza utakatifu wa maisha ya mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Uhai wa mwanadamu unatishiwa na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Mama Kanisa daima ameendelea kuwachangamotisha waamini na watu wenye mapenzi mema kusimama kidete dhidi ya utamaduni wa kifo!

Ni maneno ya Monsinyo Jean Marie Mupendawatu, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa wahudumu wa sekta ya afya. Anasema, Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro alijipambanua kuwa ni mtetezi na mtangazaji wa Injili ya Uhai inayoendelea kuwekwa rehani kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia katika tiba ya mwanadamu. Waraka wa kichungaji wa Injili ya Uhai uliotolewa na Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa pili ni jibu makini katika kushughulikia changamoto dhidi ya utamaduni wa kifo.

Magonjwa na mateso ya mwanadamu yanaonekana kuwa ni mzigo usioweza kubebeka kiasi hata cha kuhatarisha utakatifu na thamani kubwa ya maisha ya mwanadamu na matokeo yake ni baadhi ya watu kutaka kukumbatia utamaduni wa kifo! Hapa mwanadamu anashikwa na kigugumizi na kushindwa kutambua kwamba, maisha yake ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwamba, ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Maisha ya mwanadamu daima yana uhusiano na uwepo wa Mwenyezi Mungu.

Monsinyo Mupendawatu anasema, hakuna mtu au serikali yenye mamlaka ya kunyofoa maisha ya mtu! Sheria zinazokumbatia Eutanasia na utoaji mimba ni kinyume cha Injili ya Uhai. Hiki ni kishawishi cha binadamu cha kujifanya kuwa ni mmiliki wa hatima ya maisha yake, jambo ambalo kimsingi si kweli! Vitendo hivi ni mauaji ya makusudi ambayo ni kinyume cha haki, sheria na utashi wa Mungu kwa binadamu.

Huduma ya tiba kwa mwanadamu inapaswa kutekelezwa kwa kuongozwa na kanuni maadili, sheria na dhamiri nyofu. Kuna baadhi ya tiba zilizoendelea zinazotolewa kwa wagonjwa kiasi kwamba, unakuwa ni mzigo kwa mgonjwa na familia yake, lakini wahudumu wa afya wanaendelea kuitoa wakati mwingine kwa ajili ya mafao yao binafsi au tafiti wanazofanya! Teknolojia ya kisasa katika tiba itumike kwa busara na hasa kama kunaonekana kwamba, kuna dalili kwa mgonjwa kuweza kupata nafuu katika mateso na mahangaiko yake.

Monsinyo Mupendawatu anasema katika baadhi ya nchi kuna wosia unaotolewa na mgonjwa wa kukataa kula chakula au kupewa dawa fulani kama njia ya kutema zawadi ya uhai. Hapa Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita alionya kwamba, ni kitendo cha mwanadamu kutaka kujikuza kwa kuelemewa na ubinafsi na uhuru usiokuwa na mipaka. Hapa waamini na watu wenye mapenzi mema wanapaswa kuwa makini ili kufahamu Mafundisho Jamii ya Kanisa kuhusiana na mambo ya tiba: Mgonjwa kimsingi ana haki ya kupata chakula, maji na tiba muafaka kadiri ya hali yake.

Monsinyo Mupendwatu anahitimisha tafakari hii kwa kusema kwamba, Waraka wa Injili ya Uhai umekuwa ni dira na mwongozo kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai dhidi ya Utamaduni wa kifo. Kwa hakika haya ni mapinduzi ya kitamaduni yaliyofanywa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili. Waamini wanapaswa kuendeleza dhamana hii kwa kuwa na majiundo makini ya dhamiri nyofu inayoheshimu na kuthamini uhai wa binadamu kama zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.