Makanisa yanapania kuona kwamba, tunu ya maisha, haki na utu wa mwafrika vinadumishwa
Shirikisho la Mabaraza ya Makanisa Barani Afrika linaadhimisha Jubilee ya miaka 50
tangu lilipoanzishwa nchini Uganda kunako mwaka 1963, wakati ambapo nchi nyingi za
Kiafrika zilikuwa zinajitwalia uhuru wake wa bendera. Kilikuwa ni kipindi cha mapambano,
kinzani na mikakati ya kuondokana na ujinga, umaskini na magonjwa kwa kuhakikisha
kwamba, Bara la Afrika linatumia rasilimali zake kikamilifu kwa ajili ya ustawi na
maendeleo ya watu wake.
Mkutano wa kumi wa Shirikisho la Mabaraza ya Makanisa
Barani Afrika uliokuwa unaongozwa na kauli mbiu "Mungu wa uhai, liongoze Bara la Afrika
katika haki, amani na utu", ulikuwa ni fursa kubwa kwa wajumbe kuchangia kwa kina
na mapana umuhimu wa tunu hizi kwa ajili ya mchakato wa maendeleo endelevu yanayogusa
mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili Barani Afrika.
Itakumbukwa kwamba,
maadhimisho haya kikanda ni sehemu ya maandalizi ya Mkutano mkuu wa Baraza la Makanisa
Ulimwenguni utakaofanyika kuanzia tarehe 30 Oktoba hadi tarehe 8 Novemba 2013 mjini
Busan, Korea ya Kusini.
Askofu mkuu Valentine Mokiwa, Mwenyekiti wa Shirikisho
la Makanisa Barani Afrika amesema kwamba, kuanzishwa kwa Shirikisho hili kulipania
kwa namna ya pekee kuhakikisha kwamba, tasaufi ya Kiafrika inamwilishwa katika masula
ya: kijamii, kisiasa, kimaadili na kiutu ili kuleta mabadiliko yaliyokuwa yanakusudiwa
Barani Afrika baada ya kuanguka kwa ukoloni na kuanza kuibuka kwa ukoloni mamboleo.
Askofu
mkuu Mokiwa anawataka wajumbe wa Shirikisho kuendelea kusimama kidete kupambana na
baa la umaskini kwani hii ni dhambi na kashfa katika Karne ya ishirini na moja.
Kwa
upande wake, Dr. Olav Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni ameyataka
Makanisa Barani Afrika kushikamana kwa dhati na kuendelea kuwa ni sauti ya wanyonge
dhidi ya ukosefu wa haki msingi na vitendo vya uvunjifu wa misingi ya amani na utulivu.
Bara la Afrika lina utajiri mkubwa wa rasilimali na maliasili, lakini kwa
bahati mbaya, utajiri wote huu kwa miaka mingi umeendelea kuwanufaisha watu wachache
katika Jamii wakati ambapo kuna mamillioni ya watu wanateseka kwa baa la njaa, magonjwa
na umaskini. Hii ni changamoto ya kusimama kidete kutetea haki ya kiuchumi, jambo
linaloungwa mkono na Baraza la Makanisa Ulimwenguni. Kuna haja ya kubadili mwelekeo
wa sasa ambao umeligeuza Bara la Afrika kuwa ni mpokeaji wa misaada kutoka nje na
badala yake liwe ni mdau wa shughuli za kiuchumi ili kujenga na kuimarisha haki, amani
na utu!
Baadhi ya wajumbe wamesema kwamba, kuna haja kwa Makanisa kuwekeza
kwa vijana na wanawake Barani Afrika ili waweze kushiriki kikamilifu katika ustawi
na maendeleo ya Bara la Afrika, kwa kuchangia kwa hali na mali karama na mapaji ambayo
wamekirimiwa na Mwenyezi Mungu, yanayopaswa kutumiwa kwa ajili ya mafao ya wengi.
Vijana wa Kiafrika wajiamini na kujiwekea mikakati ya maendeleo badala ya
kuingiwa na kishawishi cha kutaka kuzamia ughaibuni kwa kudhani kwamba, huko kuna
kula kuku kwa mirija, lakini wanapofika Ughaibuni wanakumbana na adha ya maisha na
hali ya kukata tamaa! Ni mwaliko kwa Serikali Barani Afrika kukomesha ajira za watoto
wadogo hasa huko Sierra Leone, DRC na baadhi ya nchi za Kiafrika.
Nchi nyingi
za Kiafrika zilizoko Kusini mwa Jangwa la Sahara zimefanya maboresho katika misingi
ya demokrasia na utawala bora; zinaendelea kupembua kuhusu mikataba pamoja na kufanya
maboresho katika huduma za kijamii hususan katika sekta ya elimu na afya.