Kongamano la 51 la Ekaristi Takatifu Kimataifa kufanyika mjini Cebu, Ufilippini, Januari
2016!
Kardinali Tarcisio Bertone Katibu mkuu wa Vatican anasema kwamba, Baba Mtakatifu Francisko
ameridhia kauli mbiu ya Maadhimisho ya Kongamano la 51 la Ekaristi Takatifu Kimataifa
litakalofanyika mjini Cebu, nchini Ufilippini kunako mwaka 2016. Maadhimisho haya
yatafanyika kuanzia tarehe 25 hadi tarehe 31 Januari 2016 kwa kuongozwa na kauli mbiu
"Kristo ndani yenu, tumaini la utukufu" Wakolosai 1: 27.
Uchaguzi wa mahali
ambapo Kongamano la Ekaristi Takatifu Kimataifa lingefanyika ulitolewa na Baba Mtakatifu
mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika ujumbe wake kwa njia ya video wakati wa kufunga
Maadhimisho ya Kongamano la 50 la Ekaristi Takatifu Kimataifa lililofanyika mjini
Dublin, mwezi Juni 2012.
Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita,
aliwasihi waamini na watu wenye mapenzi mema nchini Ufilippini kuanza maandalizi mara
moja kwa ajili ya maadhimisho haya, kama sehemu ya mchakato wa kupyaisha maisha ya
Kikristo nchini humo na kwa wale wote watakaoshiriki kwa namna mbali mbali.
Ni
matumaini ya Baraza la Maaskofu Katoliki nchini Ufilippini kwamba, Maadhimisho ya
Kongamano la Ekaristi Takatifu kimataifa nchini mwao, itakuwa ni fursa makini katika
jitihada za kukuza na kuimarisha Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu nchini humo sanjari
na Maadhimisho ya Miaka 500 tangu walipoinjilishwa kwa mara ya kwanza.
Hii
ni changamoto ya kudumisha mchakato wa Uinjilishaji, ari na moyo wa kimissionari ili
kumshuhudia Kristo kwa kina na mapana zaidi. Maadhimisho haya yatakuwa ni zawadi kubwa
kwa vijana Barani Asia kutambua dhamana na wito wao katika azma ya uinjilishaji wa
kina.