Watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi wanahitaji faraja, upendo, huruma na kusaidiwa
ili kuondokana na hali hii!
Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wahamiaji na watu wasiokuwa
na makazi maalum kunako mwaka 2012 liliendesha mkutano wa shughuli za kichungaji kwa
ajili ya watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi Barani Afrika. Mkutano huu uliwashirikisha
wajumbe 88 kutoka ndani na nje ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika
na Madagascar, SECAM.
Askofu Michael
Msonganzila wa Jimbo Katoliki Musoma, ni kati ya wajumbe waliohudhuria mkutano huu
uliofanyika kwenye Makao Makuu ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Jijini Dar
es Salaam. Anasema, watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi wanahitaji faraja
na upendo kutoka kwa wadau mbali mbali. Hawa ni matokeo ya mtu binafsi, kumong'onyoka
kwa misingi ya maadili, utu wema na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano
wa Mungu. Ni watoto wanaokabiliana na hatari nyingi katika maisha yao.
Askofu
Msonganzila anaendelea kusema kwamba, kinzani, migawanyiko na mafarakano katika familia;
baadhi ya watu kushindwa kuzingatia: tamaduni,mila na desturi njema za Kiafrika ni
kati ya mambo ambayo yamepelekea kwa watoto wengi kujikuta wakiiishi nje ya mipaka
ya maisha na tunu za kifamilia; hawa ndio watoto wale wanaoishi katika mazingira hatarishi.
Baadhi yao wamekuwa na ndoto ya kutaka kupata maisha ya hali ya juu bila kuwa na maandalizi
ya kina wala kipato. Ni watoto ambao wamejikuta wakijitumbukiza na kutumbukizwa katika
matumizi haramu ya dawa za kulevya; ukahaba na kazi za shuruti.
Askofu Michael
Msonganzila anasema, watoto hawa wanapaswa kusaidiwa ili kupambana na hali yao ya
maisha, kama ilivyotokea kwa wale wanafunzi wa Emmaus waliokuwa wakisafiri kutoka
Yerusalem kwenda Emmaus wakakutana na Yesu ambaye aliwafafanulia kuhusu utajiri uliofumbatwa
kwenye Maandiko Matakatifu. Kumbe, Neno la Mungu linapaswa kuwa ni dira katika kujitambua,
kuchambuliwa na kuchambuana; ili waamini waweze kulipokea, kulikubali na kulimwilisha
katika maisha na vipaumbele vyao.
Wadau mbali mbali katika malezi na makuzi
ya watoto wanatambua kwamba, watoto hawa wanahitaji kuonjeshwa upendo unaobubujika
kutoka kwa Kristo na Kanisa lake, hata katika mazingira haya hatarishi, kwani pengine
hawa ni matokeo ya dhambi jamii; athari za uchumi, kinzani na migogoro ya kifamilia
na kijamii; kisiasa na kielimu. Watoto hawa wanahitaji kupendwa na kuthaminiwa kama
alivyofanya Msamaria mwema.
Jamii ioneshe huruma pamoja na kuibua mbinu mkakati
wa kuwasaidia ili waweze kuondokana na hali yao mbaya. Inasikitisha kuona na kusikia
kwamba, watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi wanatumiwa pia kwa ajili ya kuendeleza
biashara haramu ya dawa za kulevya pamoja na ukahaba, mambo ambayo yanaendelea kuwadidimiza
na kuwaangamiza.
Askofu Michael Msonganzila wa Jimbo Katoliki Musoma anasema,
nchi nyingi za Bara la Afrika zimekuwa ni soko na njia za biashara haramu ya binadamu,
changamoto kwa vyombo vya ulinzi na usalama kujipanga vyema ili kuzuia na kudhibiti
biashara hii haramu inayodhalilisha utu na heshima ya binadamu. Haya pia ni mambo
ambayo yanajadiliwa katika Maadhimisho ya Sinodi ya kwanza ya Jimbo Katoliki Musoma,
Tanzania.