2013-06-12 08:31:39

Wajumbe wa mkutano wa IV Kimataifa kujadili kuhusu mtoto kama mtu na mgonjwa mjini Vatican!


Mfuko wa Msamaria mwema, Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wafanyakazi katika sekta ya afya, kuanzia tarehe 14 hadi tarehe 15 Juni 2013 utaendesha mkutano wa nne wa kimataifa unaojadili kuhusu "mtoto kama mtu na mgonjwa: mchakato wa tiba linganishi". Mkutano utafunguliwa kwa Ibada ya Misa Takatifu itakayofanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Ijumaa asubuhi, tarehe14 Juni 2013.

Askofu mkuu Zygmunt Zimowski atafungua mkutano huu ili kutoa nafasi kwa mabingwa wa masuala ya tiba linganishi kutoka sehemu mbali mbali za dunia kuchangia: weledi, ujuzi na mang'amuzi yao katika kumhudumia mtoto kama mtu na mgonjwa. Mabingwa hawa wataangalia magonjwa ya afya ya akili ya mtoto na maendeleo yake; watoto wenye saratani; tiba kwa watoto wadogo kiakili: madhara na faida zake.

Majadiliano yote haya yanaongozwa na kanuni maadili "usiumize". Madawa mamboleo: faida na mapungufu yake. Wajumbe pia watagusia umuhimu wa familia katika kutibu magonjwa ya afya ya akili.Wajumbe pia watapata fursa ya kujadili masuala haya katika vikundi pamoja na kushirikishana mang'amuzi yao.

Askofu Nicolas Djomo Lola, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki DRC ataratibu majadiliano kuhusu tiba ya mtoto mgonjwa na mwelekeo wa jumla. Dr. Angela Anene Okolo kutoka Nigeria atazungumzia uhusiano uliopo kati ya Daktari na mtoto mgonjwa. Wajumbe pia watakutana kwa uwakilishi wa Mabara ili kwa pamoja waweze kujadili huduma ya tiba kwa watoto kama changamoto kwa Kanisa na Jamii: mang'amuzi na ushuhuda kutoka kwa baadhi ya Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.