2013-06-12 10:11:00

Siku ya Familia Jimbo Katoliki Murang'a Kenya


Umuhimu wa Familia umebainishwa kwa kina na mapana katika Maandiko Matakatifu. Ni katika familia mtu hujifunza upendo na uaminifu kwa Mungu na jirani. Hii ni jumuiya ya kwanza na asili ya binadamu; yenye haki na wajibu wake katika Jamii. Familia inauhusiano wa pekee katika uhai wa mwanadamu, kwani familia ni chimbuko la uhai na mapendo; mahali pa kukuza na kudumisha: ukarimu, umoja na mshikamano. Kimsingi familia ni kiini cha jamii, kumbe wadau mbali mbali wanawajibika kuziwezesha familia ili ziweze kutekeleza wajibu wake msingi katika Jamii.

Familia ni hekalu ya uhai na chembe hai ya jamii na ya Kanisa katika ujumla wake. Ni mahali panapofaa kujifunza na kuzoeshwa utamaduni wa msamaha, amani na upatanisho. Ni mahali ambapo wanafamilia wanaonja na kuonjeshana: haki, upendo, kazi, wajibu na mamlaka. Familia ni mahali pa kukuza na kuimarisha maisha ya kikristo kwa njia ya Sala, Sakarementi, Neno la Mungu na matendo ya huruma. Kimsingi familia kama anavyosema Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto wa kumi na sita ni mahali pa kuinjilisha na kujiinjilisha ili kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa.

Haya ni kati ya mambo msingi yaliyopelekea Jimbo Katoliki la Murang'a, nchini Kenya kuanzisha na kuadhimisha Siku ya Familia Kijimbo, ambayo kwa mwaka huu imefanyika hapo tarehe 9 Juni 2013 na kuongozwa na Askofu mkuu Charles Daniel Balvo, Balozi wa Vatican nchini Kenya. Askofu James Wainaina wa Jimbo Katoliki la Murang'a ndiye aliyekuwa mwenyeji wa maadhimisho haya.

Askofu mkuu Balvo anawataka waamini kushikamana kwa dhati katika maisha na tunu msingi za kifamilia, wakitambua kwamba, wao ni Familia ya Mungu inayowajibika, kama walivyobainisha Mababa wa Sinodi ya kwanza ya Maaskofu wa Afrika. Katika Ibada hii ya Misa Takatifu, wanandoa walirudia kwa mara nyingine tena ahadi na uaminifu wao katika maisha ya ndoa.

Askofu James Wainaina anasema, Jimbo limejiwekea mkakati wa ujenzi wa kituo cha mapumziko kwa ajili ya wanandoa, kinachotarajiwa kuzinduliwa mwezi Agosti, 2013. Hapa patakuwa ni mahali ambapo, wanandoa watapata nafasi ya kupumzika, kusali na kutafakari kuhusu maisha na utume wao ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla.

Askofu Charles Daniel Balvo ameendelea kuwahimiza waamini kusali kwa ajili ya kumwombea Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wake, kwani hii ni dhamana nyeti inayowajibisha sana.







All the contents on this site are copyrighted ©.