2013-06-12 09:23:33

Mwamini anahitaji mwanga wa imani ili aweze kutembea katika hija ya mwanga wa maisha ya Kikristo, kielelezo cha Sakramenti ya Ubatizo!


Baba Mtakatifu Francisko ametuma ujumbe kwa Chama cha Vipofu Italia, wakati huu ambapo kuna kundi la wazee 75 wenye upofu wanaojipumzisha kidogo na kufanya mazoezi kwenye ufuko wa Bahari mjini Tirrenia.

Baba Mtakatifu anawashukuru wazee hawa kwa kumkumbuka na kumwombea katika sala zao na kwamba, Yesu alionesha upendeleo wa pekee kwa watu waliokuwa na upofu, akawaponya na kuwapatia zawadi ya imani. Kila mwamini anahitaji kupata mwanga wa imani, ili kutembea katika hija ya mwanga wa maisha ya Kikristo inayopata chimbuko lake katika Sakramenti ya Ubatizo.

Baba Mtakatifu anawaombea wazee hawa ili waweze kuimarika katika imani; wakiwa na mwanga wa uwepo wa Mungu katika mioyo yao; mwanga ambao ni upendo unaotoa maana ya maisha, unawaangazia na kuwapatia waamini matumaini na wema kwa ajili ya jirani.

Anawatakia kila la kheri na baraka kwa kuendelea kuhimiza umuhimu wa kujenga na kudumisha utamaduni wa kukutana, upendo na mshikamano hasa kwa walemavu, ili nao pale inapowezekana waweze kushiriki katika maisha ya kijamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.