2013-06-11 09:11:28

Askofu mkuu Justin Welby kukutana na kusali pamoja na Papa Francisko, tarehe 14 Juni 2013 mjini Vatican


Baraza la Kipapa la uhamasishaji wa umoja wa Wakristo linasema, Askofu mkuu Justin Welby wa Jimbo kuu la Cantebury na Kiongozi mkuu wa Kanisa Anglikani duniani, anatarajiwa kumtembelea Baba Mtakatifu Francisko, mjini Vatican hapo tarehe 14 Juni 2013. Hii itakuwa ni ziara fupi lakini yenye umuhimu wa pekee kwa viongozi hawa wawili wa Makanisa, kwa kuwa watakutana na kuzungumza kwa pamoja, tangu wote wawili walipopewa dhamana ya kuongoza Makanisa yao.

Kwa pamoja wataangalia tena uhusiano wa kiekumene ulipo kati ya Kanisa Anglikani na Kanisa Katoliki; haki jamii, kanuni maadili, sheria na kanuni za soko la fedha kimataifa zinazopaswa kuzingatiwa ili kuwaletea watu maendeleo endelevu. Askofu mkuu Welby tangu aingie kwenye madaraka ametoa kipaumbele cha pekee katika kukuza na kudumisha upatanisho sanjari na kuhakikisha kwamba, kinzani na migogoro ndani ya jamii inapatiwa ufumbuzi wa kudumu.

Baba Mtakatifu Francisko kwa upande wake, anahimiza watu kujenga madaraja ya upendo na mshikamano kati ya watu wa Mataifa, ili wote waweze kutambuana kama ndugu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Kanisa Anglikani na Kanisa Katoliki yamekuwa na ushirikiano wa karibuni nchini Uingereza hasa kwa kusimamia tunu msingi za maisha ya ndoa na familia sanjari na tunu msingi za kijamii zinazopaswa kudumishwa kwa ajili ya mafao ya wengi, ustawi na maendeleo ya jamii. Katika ziara hii fupi, Askofu mkuu Welby atafuatana na Askofu mkuu Vincent Nichols, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza.

Baba Mtakatifu Francisko na mgeni wake mara baada ya hotuba, wakati wa mchana kwa pamoja watasali. Askofu mkuu Welby atapata pia fursa ya kutembelea Kanisa kuu la Mtakatifu Petro hadi chini kabisa ya Kanisa, kama alivyofanya mtangulizi wake, Askofu mkuu mstaafu Rowan Williams alipotembelea Roma kwa mara ya kwanza.

Askofu mkuu Welby ameomba pia nafasi ya kusali kwenye kaburi la Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili na atatembelea Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Umoja wa Wakristo, chini ya uongozi wa Kardinali Kurt Koch.







All the contents on this site are copyrighted ©.