Utata kwa Padre Malumalu kuteuliwa kuwa Rais wa Tume huru ya uchaguzi DRC!
Hivi karibuni Padre Appolinaire Malumalu alichaguliwa na kuwa Rais wa Tume huru ya
uchaguzi nchini DRC na Bunge la DRC. Itakumbukwa kwamba, alikuwa pia ni Rais wa Tume
ya Uchaguzi DRC iliyosimamia uchaguzi mkuu uliofanyika kunako mwaka 2006. Padre Malumalu
amechaguliwa kutoka katika kundi la “madhehebu ya kidini” kwa niaba ya vyama vya kiraia.
Wachunguzi wa masuala ya kisiasa nchini DRC wanasema, Padre Malumalu alionesha
uwezo mkubwa katika kuratibu mchakato mzima wa uchaguzi mkuu kwa mwaka 2006 na matokeo
yake yanaonekana. Lakini, Baraza la Maaskofu Katoliki DRC mapema mwaka huu lilionya
juu ya Mapadre na Watawa kujihusisha na masuala ya kisiasa kwani ni kinyume cha sheria
za Kanisa na kutokana na mantiki hii, Padre Malumalu anakwenda kinyume cha sheria
na taratibu zilizowekwa na Baraza la Maaskofu Katoliki DRC.