Mwilisheni Ibada ya Misa Takatifu katika maisha; Jengeni utamaduni wa kuabudu Ekaristi
Takatifu na Kupokea Sakramenti ya Upatanisho!
Baraza la Maaskofu Katoliki Ujerumani, Jumapili tarehe 9 Juni 2013 limehitimisha Maadhimisho
ya Kongamano la Ekaristi Takatifu Kitaifa, lililokuwa linaadhimishwa Jimbo kuu la
Colony nchini Ujerumani.
Katika Maadhimisho haya, Baba Mtakatifu amewakilishwa
na Kardinali Paul Joseph Cordes, Rais mstaafu wa Baraza la Kipapa linalo ratibu misaada
ya Kanisa Katoliki, Cor Unum. Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu imekuwa ikifanyika
Jimboni humu tangu karne ya kumi na tatu na Siku kuu ya Ekaristi Takatifu imekuwa
ikiadhimishwa kwa Ibada na Maandamano makubwa.
Baba Mtakatifu katika ujumbe
wake kwa Maadhimisho haya anasema kwamba, anapenda kuungana na Waamini wa Kanisa Katoliki
nchini Ujerumani kuonesha umoja wa Kanisa la Kiulimwengu. Mitume walitambua na kuonja
njaa ya mwili, iliyowasaidia kujenga na kuimarisha uhusiano wa dhati na Yesu wa Nazareti,
wakaimarishwa katika hija ya imani ambayo inawakirimia maisha tele!
Baba Mtakatifu
anawaalika waamini wa nyakati hizi kumwendea na kujenga urafiki na Yesu kwa njia ya:
kusikiliza kwa makini Maandiko Matakatifu, lakini kwa namna ya pekee katika Maadhimisho
ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, chanzo na kilele cha maisha na utume wa Kanisa ambao
ni mwendelezo wa kazi ya ukombozi na maboresho ya maisha ya kiroho kwa njia ya upendo
unaobubujika kutoka kwa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.
Baba
Mtakatifu anawataka waamini kujifunza namna ya kumwilisha Ibada ya Misa Takatifu katika
maisha yao, kujenga utamaduni wa kumwabudu Yesu katika Sakramenti Kuu pamoja na kupokea
Sakramenti ya Upatanisho mara kwa mara. Kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, mlango
wa imani, waamini wamebahatika kuwa ni ndugu zake Yesu Kristo na kwa njia ya Ekaristi
Takatifu wanakirimiwa nguvu na ujasiri wa kuendeleza mchakato wa kazi ya Ukombozi.
Baba
Mtakatifu Francisko anawachangamotisha waamini kumtolea Kristo ushuhuda wa maisha
yao; kwa kutangaza kile walichoona na kusikia kwamba, Yesu anayo maneno ya uzima.Familia
ya Mungu inawajibu wa kumpeleka Mungu duniani na dunia kwa Mungu. Kukutana, kujiaminisha
na kumtangaza Kristo ni mihimiri mikuu ya imani inayojielekeza zaidi katika Fumbo
la Ekaristi Takatifu. Maadhimisho ya Kongamano la Ekaristi Takatifu Kitaifa katika
Mwaka wa Imani ni kutangaza kwa furaha uwepo endelevu wa Kristo ndani ya Kanisa lake.