2013-06-10 07:14:41

Askofu Mkude: Umuhimu wa Neno la Mungu na Maisha ya Kisakramenti


Waamini wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, wanajitahidi kulisoma, kulitafakari na kulimwilisha Neno la Mungu katika maisha na vipaumbele vyao. Neno la Mungu liwaweze waamini kuwa kweli ni vyombo vya haki, amani na upatanisho. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika Waraka wake wa kichungaji, Dhamana ya Afrika, anawahimiza Waamini kushiriki kikamilifu katika utume wa Biblia kwa kuanzia ndani ya Familia.

Katika sehemu hii ya pili ya Mahojiano kati ya Radio Vatican na Askofu Telesphor Mkude, Mwenyekiti wa Idara ya Familia, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania anaendelea kukazia umuhimu wa Neno la Mungu katika maisha na utume wa Familia za Kikristo, changamoto na mwaliko kwa waamini kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu. Hapa ni mahali ambapo Neno la Mungu linasomwa, linafafanuliwa, linatafakariwa kwa pamoja na kumwilishwa kwa njia ya matendo.

Askofu Mkude anasema kwamba, kuna haja ya kuendelea kuimarisha Katekesi kuhusu Fumbo la Ekaristi Takatifu chanzo na kilele cha maisha na utume wa Kanisa; kumbu kumbu endelevu ya Sadaka ya Kristo Msalabani, Ishara ya Umoja na Kifungo cha Upendo, Karamu ya Pasaka na amana ya uzima wa milele. Waamini wanapompokea Yesu Kristo katika Ekaristi takatifu wanashirikishwa Umungu wa Kristo kama Yeye mwenyewe alivyoshiriki ubinadamu kwa njia ya Fumbo la Umwilisho.

Askofu Telesphor Mkude anasema kwamba, kwa njia ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, waamini wanapata ujasiri, nguvu, ari na moyo wa kuweza kumtolea ushuhuda Kristo na Kanisa lake kwa njia ya imani katika matendo. Anasema Askofu Mkude, huu ni mwaliko kwa waamini kuwa kweli ni chombo cha: haki, amani, upendo, mshikamano na upatanisho wa kweli.

Kimsingi, Uelewa wa Neno la Mungu na Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu yawachangamotishe waamini kuwa kweli ni vyombo vya haki, amani na upatanisho kama wanavyokazia Mababa wa Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika.








All the contents on this site are copyrighted ©.