2013-06-08 10:44:45

Jubilee ya miaka 100 ya Ukristo Parokia ya Mtakatifu Boniface Aluor, Jimbo kuu la Kisumu!


Parokia ya Mtakatifu Boniface Aluor, Jimbo kuu la Kisumu, Kenya hivi karibuni imeadhimisha Jubilee ya miaka 100 tangu ilipoanzishwa kunako tarehe 5 Juni 1913, ikiwa ni Parokia ya kwanza kabisa kuanzishwa katika eneo la Waluo. Parokia hii imebahatika kupata Parokia nyingine 19 zilizozaliwa kutoka kwenye Parokia hii mama! Jubilee ya Miaka 100 ya Parokia ya Mtakatifu Boniface imehudhuriwa na Askofu mkuu Charles Daniel Balvo, Balozi wa Vatican nchini Kenya.

Katika hotuba yake, Askofu mkuu Zacchaeous Okoth wa Jimbo kuu la Kisumu, amewashukuru kwa namna ya pekee Wamissionari wa Mill Hill, waliojitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu na matunda yake yanaonekana. Askofu mkuu Okoth amewashukuru pia Mapadre Wazalendo waliondeleza kazi ya Uinjilishaji kama sehemu ya mchakato wa ujenzi wa Ufalme wa Mungu.

Jubilee hii imepambwa kwa Majandokasisi wanane kupewa Daraja la Ushemasi, kielelezo cha huduma ndani ya Kanisa. Kigango cha Mtakatifu Pantalion kimepandishwa hadhi na kuwa ni Parokia Mpya na Padre Paul Oduor ameteuliwa kuwa ni Paroko wake wa kwanza.

Askofu mkuu Balvo katika mahubiri yake, amewataka Mashemasi wapya kujitosa kimaso maso kutangaza Injili ya Kristo hadi miisho ya dunia. Watambue kwamba, kwa Daraja la Ushemasi, wanakuwa ni sehemu ya wajenzi wa Ufalme wa Mungu uliojionesha kwa namna ya pekee kwa njia ya Sadaka ya Kristo Msalabani. Kama Mashemasi wanaitwa na kutumwa kumhudumia Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 100 ya Parokia ya Mtakatifu Boniface Aluor sanjari na Mwaka wa Imani, yawe ni kikolezo cha imani tendaji katika maisha na vipaumbele vya waamini wa Jimbo kuu la Kisumu, Kenya.







All the contents on this site are copyrighted ©.