2013-06-07 09:30:17

Shika kitakatifu siku ya Mungu


Baba Mtakatifu Francisko kwa mara ya kwanza anatarajiwa kushiriki katika mjadala kuhusu Amri 10 za Mungu, tukio ambalo limeandaliwa na Chama cha Kitume cha Uamsho wa Roho Mtakatifu kwa kutuma ujumbe kwa njia ya video, Jumamosi, tarehe 8 Juni 2013. Tukio hili linafanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Jimbo kuu la Milani, Kaskazini mwa Italia. Wakati huu, washiriki wa kongamano hili wanajadili kuhusu Amri ya Tatu: Shika kitakatifu siku ya Mungu.

Yote haya ni matukio yanayokwenda sanjari na changamoto ya Uinjilishaji Mpya iliyotolewa na Mama Kanisa wakati huu wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani na yatafanyika sehemu mbali mbali za Italia. Itakumbukwa kwamba, kwa mara ya kwanza Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kunako Mwezi Septemba 2012, alizindua Maadhimisho haya mjini Roma, kwa kujadili Amri ya Kwanza "Ndimi Bwana Mungu wako, usiabudu Miungu wengine".

Baadaye tarehe 15 Septemba 2012 maadhimisho haya yalifanyika mjini Verona kwa kutafakari Amri ya pili "Usilitaje bure jina la Mungu wako". Mjini Napoli, wao walitafakari Amri ya Nne "Waheshimu Baba na Mama Upate Miaka mingi na heri duniani". Ni kongamano ambalo linawashirikisha watu kutoka medani mbali mbali za maisha.







All the contents on this site are copyrighted ©.