Tanzania na Singapore kuendelea kushirikiana katika nyanja mbali mbali
Singapore itaendelea kuisaidia Tanzania Katika jitihada zake za kuinua elimu na kuongeza
ujuzi kwa Watanzania zaidi kupitia mpango wake wa kutoa fursa za mafunzo kwa nchi
zinazoendelea. Rais wa Singapore Dr. Tony Tan Keng Yam amemuambia Rais Jakaya Mrisho
Kikwete Jumatatu katika ikulu ya Singapore maarufu kama Istana. "Hatuna Maliasili
hivyo tumewekeza zaidi katika elimu na mafunzo kuanzia shuleni, vyuo vya ufundi na
vyuo vikuu, tuko tayari kushirikiana na Tanzania katika hili" Dr. Tan amesema.
Singapore
inasifika kote duniani kwa juhudi zake chini ya Waziri Mkuu wake wa kwanza Bwana Lee
Kuan Yew ambaye aliwekeza na kukazania zaidi elimu ya watu wake kitu ambacho kimesaidia
nchi ya Singapore kutoka dunia ya tatu hadi dunia ya kwanza kiuchumi. Rais Kikwete
amewasili Singapore amewasili akitokea Japan ambapo amehudhuria mkutano wa Tokyo
unaozungumzia maendeleo ya Afrika -Tokyo International Conference on Africa Development.
Akiwa
nchini Singapore Rais Kikwete amekutana na wafanyibiashara na kuwakaribisha Tanzania
kwa ajili ya uwekezaji ambapo wakuu wa taasisi na sekta mbalimbali wamepata nafasi
kuelezea fursa na nafasi za uwekezaji nchini. Rais pia ameshuhudia utiaji saini wa
mikataba kadhaa ya ushirikiano kati ya Tanzania na Singapore.
Mikataba
iliyotiwa saini ni ile ya shirikisho la wafanyabiashara wa Singapore na mfuko wa Sekta
binafsi Tanzania(TPSF), Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) na Shirika la Intrasia
Capital wanaoshughulikia mambo ya nishati, Mamlaka za Bandari Tanzania na Singapore,
na kampuni binafsi za Tanzania na Singapore (Pacific International Line ya Singapore
na Mac Group ya Tanzania. Rais Kikwete pia ametembelea bandari ya Singapore, Mojawapo
ya bandari tano duniani zinazoongoza kwa utendaji wake bora
Rais pia anatarajia
kutembelea Shirika la Nyumba na Maendeleo ya Mji ambalo linasifika kwa kuendeleza
miji, ujenzi wa nyumba na makazi ya bei nafuu. Shughuli zingine ambazo Rais amefanya
ni kutembelea Chuo cha Ufundi cha Singapore na kutembelea maeneo ya viwanda na biashara.
Katika ujumbe wake Rais ameambatana na mawaziri wanao shughulikia maeneo ambayo atatembelea
ambayo ni Waziri wa Mambo ya Nje Benard Membe, Waziri wa Viwanda Dr. Abdalah Kigoda,
Waziri wa Ardhi na Makazi Prof. Anna Tibaijuka ,Waziri wa Uchukuzi Dr. Harrison Mwakyembe
na Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi Zanzibar Rashid Seif Suleiman.
Wapo pia
watendaji wakuu wa mashirika yakiwemo kituo cha uwekezaji nchini cha Tanzania bara
na cha Zanzibar (TIC) Na (ZIPA), Shirika la Nyumba (NHC) , Bandari , Shirika la
Maendeleo (NDC), Sekta binafsi na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara (TANTRADE). Wengine
ni Shirika la Maendeleo ya Petroli Nchini (TPDC), Kituo cha Maeneo huru ya Uwekezaji
(EPZA) na Chama cha Biashara, Viwanda na Kilimo (TCCIA) Chama cha Wafanyibiashara
Wanawake Tanzania (TWCC) Chama cha Wanawake wanaojishughulisha na kazi za mikono(TAWOHA),
Muungano wa Yyama vya Utalii Tanzania na wafanyibiashara binafsi.
Katika ujumbe
wake Rais pia amefuatana na Wabunge wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwemo
Mh. Hamis Kigwangala , CCM Nzega , Moses Machali NCCR-Mageuzi, Kasulu Mjini , Mohamed
Dewji CCM-Singida mjini, Mh. Silvester Koka , Kibaha Mjini na viongozi wa Manispaa
za Dar-es-Salaam, Ilala, Temeke, Kinondoni na Mbeya.