2013-06-05 07:37:18

Askofu mkuu Ruzoka: Tabia ya watu kujichukulia sheria mkononi ni hatari kwa misingi ya taifa!


Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Rasimu ya Katiba yake inabainisha misingi mikuu ya Taifa kuwa ni: uhuru, haki, udugu, usawa, umoja amani na mshikamano. Inapania kuenzi na kuzingatia Tunu za Taifa zifuatazo: utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi, uwajibikaji, na lugha ya Taifa. Watu wenye mapenzi mema na wapenda amani duniani wanaendelea kujiuliza nini ni chimbuko la watu nchini Tanzania kuanza kujichukulia sheria mikononi mwao, hali ambayo kwa sasa inaanza kuonekana kwamba inajenga mazoea. RealAudioMP3

Askofu mkuu Paul Ruzoka, Mwenyekiti wa Tume ya Haki na Amani, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania anasema, tabia hii inaleta madhara makubwa kwa wahusika wenyewe, lakini zaidi inadumaza maendeleo na hivyo kusababisha maafa na uharibifu mkubwa wa maisha na mali za watu.

Ni vitendo vinavyovuruga misingi ya haki, amani, upendo na utulivu miongoni mwa watanzani, tunu ambazo Tanzania imekuwa ikijivunia tangu ilipojipatia uhuru wake takribani miaka 51 iliyopita. Kuna haja kwa wadau mbali mbali kuchunguza kwa makini ili kubaini chanzo cha vurugu hizi.

Hata hivyo Askofu mkuu Ruzoka anabainisha kwamba, kuna haja ya kujenga na kudumisha misingi ya utawala bora; utawala unaozingatia utu na heshima ya kila mtu pamoja na sheria za nchi.

Wadau wanaohusika kusimamia na kutekeleza sheria na kanuni za utawala bora wanapaswa kutekeleza wajibu wao barabara sanjari na kudhibiti magenge ya watu wanaochochea fujo na vurugu za kijamii, ili mambo haya yasigeuke kuwa ni sehemu ya utamaduni wa watanzania. Yote haya yatekelezwe kadiri ya sheria na taratibu za nchi.








All the contents on this site are copyrighted ©.