2013-06-04 07:20:08

Huduma ya maji safi na salama pamoja na lishe bora zinahitaji mshikamano na uwajibikaji wa pamoja!


Askofu mkuu Francis Chullikatt, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa, akichangia mada kuhusu maendeleo endelevu na kwa namna ya pekee kipengele cha maji na afya anasema kwamba, hizi ni sekta zinazohitaji kuwa na mshikamano na uwajibikaji utakaowawezesha watu wengi zaidi kupata huduma hizi muhimu katika maisha ya mwanadamu. RealAudioMP3

Umefika wakati kwa Jumuiya ya Kimataifa kuona umuhimu wa kutangaza kuwa mambo haya ni sehemu ya haki msingi za binadamu, ikiwa kama Jumuiya ya Kimataifa inataka kuendeleza na kuimarisha haki msingi za binadamu na mafao ya wengi.

Ujumbe wa Vatican kwenye mkutano huu unabainisha kwamba, kwa miaka mingi umejitahidi kutoa ushawishi kwa Serikali na Jumuiya ya Kimataifa kutambua kwamba, maji na huduma msingi za afya ni kati ya haki msingi za binadamu lakini bila mafanikio, kwani Jumuiya ya Kimataifa bado inasita kuonesha msimamo wake katika mambo haya. Lakini ukweli wa mambo unaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu millioni 800 ambao hawana huduma ya maji safi na salama, ingawa maji ni sehemu ya uhai wa binadamu.

Hii ni changamoto pia kwa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, watu wanapata huduma bora za afya kama sehemu ya utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015. Takwimu zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu billioni 2.5 hawana huduma bora ya afya. Changamoto zote hizi ni fursa makini kwa Jumuiya ya Kimataifa kutoa kipaumbele cha pekee katika mikutano yake ili kubainisha mbinu mkakati utakaowawezesha watu wengi zaidi kupata haki zao msingi kwa kuwa na uhakika wa maji safi na salama pamoja na huduma bora za afya.

Askofu mkuu Chullikatt anafafanua kwamba, ili kuweza kufikia Malengo haya kuna haja kwa wadau mbali mbali kutekeleza dhamana yao kwa vitendo badala ya kuendelea kutoa ahadi za mikono mitupu! Jumuiya ya Kimataifa ibainishe ni kwa jinsi gani inaweza kutekeleza haki hizi msingi, kwa kutambua kwamba, lengo ni kumhudumia kwanza mwanadamu licha ya faida ionayoweza kupatikana katika huduma hii. Itakumbukwa kwamba, huduma ya maji safi na salama inavuka mipaka ya nchi, jambo linalohitaji kwa namna ya pekee kujenga na kuimarisha mshikamano wa kimataifa, kwa kusimamia rasilimali hii pamoja na kuwa na matumizi bora kwa ajili ya mafao ya wengi.

Hapa kuna haja ya kuunda uongozi madhubuti wa kikanda ili kuweza kukusanya nguvu ya pamoja, kwa kuzingatia: maendeleo, usawa, busara na mshikamano wa kidugu katika kuratibu matumizi bora ya maji kama sehemu ya mafao ya wengi. Wadau mbali mbali wanapaswa kushirikishwa ili kulinda na kudumisha haki ya maji, inayopaswa kutumiwa kwa busara na kuepuka uwezekano wa kutumia maji vibaya. Haki inapaswa kutumika kwa kutambua mtu, sheria na rasilimali fedha; mambo yanayopaswa kusimamiwa na kanuni ya auni ili huduma hii iweze kutolewa kwa ufanisi mkubwa.

Askofu mkuu Francis Chullikatt anabainisha kwamba, Malengo ya Maendeleo ya Millenia yanapaswa kuwa ni kikolezo kikubwa cha maboresho ya maisha ya watu, sanjari na upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama, bila kusahau huduma msingi za afya. Jumuiya ya Kimataifa ifanye juhudi za makusudi ili kuhakikisha kwamba, watu wengi wanapata huduma ya maji safi na salama, kwani hii ni sehemu ya haki zao msingi. Kuna uhusiano mkubwa kati ya maji na usalama wa chakula kwa ajili ya: maisha, ustawi na maendeleo ya binadamu. Rasilimali ya dunia itumike vyema ili kukidhi mahitaji ya kizazi cha sasa na kile kijacho.








All the contents on this site are copyrighted ©.