2013-06-03 09:51:07

Japan kuwekeza Barani Afrika katika nishati na miundo mbinu ya usafirishaji


Serikali ya Japan imeahidi kuzipatia nchi za Kiafrika msaada wa Euro billioni 24.2 katika kila kipindi cha miaka mitano kama sehemu ya mchakato wa maendeleo endelevu Barani Afrika.

Hayo yamebainishwa na Bwana Shinzo Abe, waziri mkuu wa Japan wakati wa hotuba yake ya ufunguzi wa Mkutano wa Kimataifa wa Maendeleo Afrika, TICAD, uliofunguliwa mwishoni mwa juma. Ni mkutano unaogharimiwa na Japan, Umoja wa Mataifa, Benki ya Dunia na kwa mara ya kwanza Umoja wa Afrika umeshiriki pia.

Viongozi wa Bara la Afrika wamepewa changamoto ya kuendeleza rasilimali watu, kufanya maboresho makubwa katika sekta ya afya pamoja na kuongeza tija na uzalishaji kwenye sekta ya kilimo. Haya ni maeneo makubwa yanayopaswa kufanyiwa kazi na viongozi wa Afrika kama kichocheo cha maendeleo kwa kushirikisha sekta ya umma na ile ya binafsi. Bara la Afrika linapaswa kuchukuliwa kuwa ni mdau mkubwa wa biashara na wala si tu mpokeaji wa misaada kutoka nchi za nje.

Japan inatarajia kuwekeza zaidi katika masuala ya nishati na usafirishaji Barani Afrika. Viongozi wa Afrika wamekumbushwa pia umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kudumisha haki msingi za binadamu, amani na kwamba, utulivu ni kigezo kikuu cha maendeleo Barani Afrika. Ni wajibu wa Afrika kwa kushirikiana na Jumuiya ya Kimataifa kujitahidi kudhibiti vitendo vya uharamia vinavyokamisha usafirishaji wa mizigo kwenye Bahari ya Hindi.







All the contents on this site are copyrighted ©.