2013-06-01 11:59:35

Kanisa halitaacha kutangaza Fumbo na Kashfa ya Msalaba


Kanisa ni Familia ya Mungu inayowajibika na kwamba, Wakristo hawana sababu ya kuogopa Kashfa ya Fumbo la Msalaba. Watambue kwamba, Yesu Kristo ndiye Neno aliyefanyika mwili na kukaa kwake Bikira Maria. Ni Mwana wa Mungu aliye hai na ni Mtakatifu wa Bwana. Kanisa linatambua na kuliheshimu Fumbo la Umwilisho, ambalo kwa watu wengine ni Kashfa ya Mwaka.

Ni sehemu ya mahubiri ya Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, tarehe Mosi, Juni 2013 aliyoyatoa kwenye Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae, kilichoko mjini Vatican. Kanisa linaendelea kutangaza Fumbo hili kwa njia ya maisha na utume wake. Kanisa linaonesha kwa namna ya pekee, uwepo endelevu wa Kristo miongoni mwa watu wake.

Kanisa linaungama na kukiri kwamba, Yesu ni Mwana wa Mungu aliye hai. Kwa njia hii, Wakristo kama ilivyokuwa kwa Kristo mwenyewe watakabiliana na madhulumu. Kwa hakika, Kashfa ya Msalaba ni sehemu ya maisha na utume wa Kanisa. Ikumbukwe kwamba, Kanisa si ushirika wa kitamaduni, kidini wala kijamii, bali ni Familia ya Kristo inayoendeleza utume wa Kristo hadi miisho ya dunia.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika Wakristo kushuhudia kwa maneno na matendo yao kuhusu ukweli wa Fumbo la Umwilisho: Kristo alizaliwa, akateswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu, limbuko lao waliolala katika usingizi wa amani. Kanisa kamwe halitaacha kutangaza Fumbo na Kashfa ya Msalaba. Waamini wasimame kidete kutetea na kushuhudia ukweli wa Fumbo hili.







All the contents on this site are copyrighted ©.