2013-05-31 10:07:57

Sherehe ya Mwili na Damu ya Kristo


Mpendwa mwana wa Mungu, ninakualikeni tukatafakari pamoja Neno la Mungu leo ikiwa ni sherehe ya Mwili na Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo. RealAudioMP3

Sherehe hii ni kati ya sherehe za Bwana na huadhimishwa Dominika inayofuata mara baada ya sherehe ya Utatu Mtakatifu. Ni sherehe ambayo ina uhusiano wa moja kwa moja na Alhamisi kuu ambapo fumbo la Ekaristi Takatifu linawekwa katika Kanisa na Yesu Kristu mwenyewe.

Siku ya Alhamis Kuu hatukupata nafasi ya kusherehekea hasa kwa shangwe na nderemo kwa kuwa tulikuwa tayari katika Juma Kuu, Juma la Mateso ya Bwana. Kumbe Mama Kanisa anatujalia nafasi tena ya kusherehekea na kushangilia kwa vigelegele sherehe hii hivi leo.

Ndiyo kusema katika sikukuu hii tunafanya ukumbusho wa Karamu ya mwisho, ambapo Bwana alikula karamu hiyo pamoja na wanafunzi wake. Ni katika karamu hiyo aliweka sakramenti ya Ekaristi na sakramenti ya Upadre. Mama Kanisa hufanya maandamano katika siku hii ikiwa ni ishara ya ushuhuda wa imani akitangaza ukuu wa Mungu kwa mataifa ambao hujidhihirisha kwa njia ya Ekaristi Takatifu. Ni ishara ya shukrani kwa Mungu kwa ajili ya zawadi ya Mwili na Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo. Ekaristi Takatifu ni chimbuko la Kanisa na hivi tunasherehekea na kushangilia zawadi ya Kanisa pia kama Safina ya wokovu.

Mpendwa mwana wa Mungu, tunaposherehekea Sherehe ya Mwili na Damu ya Bwana kwa shangwe Mama Kanisa atuwekea Neno la Bwana akitaka polepole kutambua hicho tunachokisherehekea ni kitu cha thamani kuu. Mwinjili Luka anakuja kwanza na maneno mawili Njaa na Jangwa. Kumbuka kunapotokea njaa katika maeneo yako, natumai mahangaiko ni makuu hata zaidi ya vita ya silaha!

Njaa yaweza kuwa chanzo cha mafarakano katika familia na imetokea hata mara kadhaa mababa wa familia kukimbia na kuziacha familia zao. Kukosa chakula, yaani kuwa katika baa la njaa yawezekana kutupa nafasi ya kufikiri juu ya thamani ya chakula na hivi tukiwanacho tukaweza kukitumia vizuri. Tukitazama njaa kiroho inawezekana ikawa ni nafasi ya kuona pia mpango wa Mungu kwetu.

Mpendwa msikilizaji, uthamani wa Ekaristi Takatifu waweza kueleweka vema kupitia mang’amuzi ya njaa! Ebu fikiria mmoja akikwambia au akisema “sina muda leo wa kwenda Misa au Misa inanichosha”. Mara moja huyu hana njaa na hajui thamani ya Misa Takatifu, hajui thamani ya Ekaristi Takatifu. Katika hali ya namna hii hata mmoja angesisitiza sheria haiwezekani kumfanya mmoja ashiriki Misa, yafaa kuwa na njaa, njaa ya Neno la Mungu, njaa ya Misa, njaa ya Ekaristi Takatifu. Lakini pia yafaa kujiuliza je ni njaa gani tunakuja nayo katika Misa?

Njaa ya kujisifu, ya kuangalia, ya kusikiliza? Au ya kushiriki mafumbo ya Mungu? Yafaa kutafakari vema aina ya njaa tunayopaswa kuwa nayo. Ni njaa ya kutaka kuchota neema kwa ajili ya kutekeleza wito wa Bwana “nendeni duniani kote mkawafanye wote kuwa wanafunzi wangu”. Ni njaa ya kutambua kuwa katika Msalaba, Bwana amemwaga Damu yake kwa ajili ya ulimwengu, kumbe njaa ni kuwa na kiu ya kupeleka ujumbe wa upendo huo kwa mataifa.

Neno la pili ni Jangwa, jaribu kufikiri juu ya jangwa yaani pale ambapo panasadikika kutokuwa na maisha. Ni neno muhimu kwa ajili ya tafakari yetu maana ni hapo Bwana analeta maisha kinyume na fikira za Mitume ambao waliona haiwezekani kufanya kitu zaidi ya kuwaaga makutano. Bwana ni chanzo cha maisha pale ambapo hatuoni mbele wala nyuma.

Ni Ekaristi Takatifu ambayo hutupa maisha katika ulimwengu wa leo ambao unaonekana kuwa Jangwa. Machafuko, mauaji, siasa mpindisho zisizojari haki na usawa wa wananchi, zisizojali huduma ya jamii ni vielelezo vya jangwa katika ulimwengu wetu. Bwana akisema heri walio maskini wa roho maana ufalme wa mbinguni ni wao, ataka daima kuleta amani itokayo katika Ekaristi kwa njia ya unyenyekevu wa moyo.

Katika jangwa anapowapa chakula anawaagiza Mitume wawaketishe watu katika safu ya watu hamsinihamsini akitaka kukuza thamani ya maisha ya pamoja na kusaidiana na kushirikishana mapendo na ndiyo maana ya kula pamoja. Bwana anatangaza kuwa Ekaristi ni sherehe ya pamoja, ni sherehe ya ushirika, upendo, umoja na mshikamano wa dhati akitaka kuondoa Jangwa na upweke katika maisha ya watu.

Mpendwa, Misa ndiyo maana yake hasa! Kwa nini wabaki nyumbani wakati Bwana akuita ukakae na wenzio katika karamu yake? Natumai pia maandamano tufanyayo yataka kuita mataifa wakatukuze ukuu wa Bwana na kwa njia ya kukaa pamoja. Maandamano yataka watu waketi katika safu, wasafiri pamoja katika safu na hivi ondoleo la upweke wa jangwani.

Mpendwa msikilizaji tunapopokea mwili na Damu ya Bwana, tunapokea mwanga katika maisha yetu maana alisema mimi ni taa ya maisha yako, ni ukweli na uzima kumbe pia twahuishwa na Bwana anayetaka toka maisha hayo tukafanye vivyo hivyo daima mpaka ajapo. Anatualika kwa njia ya Ekaristi tuishi uhuru wa wana wa Mungu aliotupatia Bwana (Lk. 4:18 na kuendelea).

Katika Injili tunayotafakari pia bado kuna jambo la msingi na la wokovu. Baada ya kuwa wamekula mkate na samaki waliweza tena kukusanya vikapu 12 vya mabaki. Hili mara moja latupa tumaini litokalo katika Bwana kuwa Bwana aliye Ekaristi haishi kamwe, ni wa milele, hutosheleza mahitaji yetu yote ya upendo jana, leo na daima (rejea maneno ya mbiu ya Yubileo Kuu ya Ukombozi mwaka 2000). Basi nasi twapaswa kuwa chemchemi ya mapendo na matumaini kwa wengine na kwa Kanisa la Kristu.

Mpendwa msikilizaji tunaposherehekea tunapaswa kufikiri kwa undani sana nini maana ya fumbo hili kuu na mwisho lazima, tafakari yetu imalizikie katika neno moja “PENDANENI KAMA NILIVYOWAPENDA NINYI”. Ninawatakieni furaha tele nikiwakumbusha fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu hadi nitakaporudi” Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.