2013-05-30 08:35:40

Maaskofu Katoliki Madagascar wanawataka wananchi wa Madagascar kusimama kidete kulinda na kutetea haki, amani na upatanisho wa kitaifa!


Baraza la Maaskofu Katoliki Madagascar hivi karibuni limehitimisha mkutano wake wa Mwaka kwa kujadili masuala kadhaa yanayogusa maisha na utume wa Kanisa nchini Madagascar, lakini kwa namna ya pekee nchi yao inapoelekea kwenye uchaguzi mkuu ambao unatarajiwa kufanyika hapo tarehe 24 Julai 2013.

Baraza la Maaskofu linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuiombea Madagascar ambayo kwa miaka ya hivi karibuni imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbali mbali, kiasi cha kuwakosesha watu amani, furaha na matumaini ya maisha. Wanawaomba waamini kushirikiana kwa pamoja kwa ajili ya kuombea amani na ufanisi katika mchakato wa uchaguzi mkuu, ili uweze kuwa huru, wa haki na uwazi bila kudanganya watu, kwani huu unaweza kuwa ni mwanzo wa mgogoro na machafuko ya kisiasa.

Maaskofu wanawaalika wananchi wa Madagascar kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi mkuu nchini humo ili kuhakikisha kwamba, wanawachagua viongozi adili watakaosimama kidete kulinda na kutetea mafao ya wengi, utu na heshima ya binadamu; viongozi ambao wanapaswa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa umoja na mshikamano wa kitaifa; viongozi ambao wataanzisha mchakato wa upatanisho ili kuganga madonda na utengano ambayo yamekuwa ni kizingiti kikubwa cha maendeleo na ustawi wa wananchi wa Madagascar.

Wananchi watataka kuona kwamba, wale watakaochaguliwa wana sifa za kuongoza, ni watu wanaoonesha uzalendo kwa nchi yao; viongozi ambao wako tayari kutumia vyema rasilimali na utajiri wa nchi kwa ajili ya maendeleo ya wengi na wala si kwa ajili ya kujinufaisha wao binafsi, ndugu, jamaa na marafiki zao kama ambavyo historia inabainisha.

Maaskofu wa Madagascar wanasikitika kusema kwamba, licha utajiri mkubwa ambao nchi yao imebahatika kuwa nao, lakini bado wananchi wake wanaendelea kuogelea katika: umaskini wa hali na kipato; magonjwa na ujinga; kinzani na migawanyiko hata ndani ya familia zenyewe; rushwa na ufisadi wa mali ya umma pamoja na ukosefu wa misingi ya haki, amani na usalama kwa raia na mali zao. Mataifa ya kigeni yamekuwa yakiingilia mambo ya ndani ya nchi ya Magagascar, hali inayoonesha kwa namna ya pekee ukosefu wa utashi wa kisiasa na uzalendo.

Baraza la Maaskofu Katoliki Madagscar, linawaalika waamini na wananchi wote wenye mapenzi mema kuanza mchakato wa upatanisho na mshikamano wa kitaifa kwa kutambua kwamba, Kanisa kama Mama na Mwalimu, linalo jukumu na dhamana ya kukemea yale yote yanayotaka kuvuruga na kuwagawa wananchi wa Madagascar, ili kuenzi na kudumisha utu na heshima ya binadamu; mafao ya wengi pamoja na ustawi wa wananchi wote wa Madagascar.

Baraza la Maaskofu Katoliki Madagscar linaliwaalika vijana kwa namna ya pekee kuwa ni wajenzi wa misingi ya haki, amani, upendo na upatanisho wa kweli na kamwe wasitumiwe na wanasiasa ucharwa kuvuruga amani nchini humo. Vijana wanachangamotishwa kuwa ni vyombo vya haki na amani na wadau wakuu wa maendeleo endelevu. Maaskofu wanawakumbusha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusali kwa ajili ya kuombea haki na amani kwa kutambua kwamba, haki ni msingi wa amani.







All the contents on this site are copyrighted ©.