2013-05-30 07:48:24

Maana ya Fumbo la Msalaba!


Msalaba ni kielelezo cha upendo, huruma na hekima ya Mungu kwa mwanadamu. Ni alama ya ushindi na matumaini, umoja na mshikamano wa dhati. RealAudioMP3

Ni maneno ya Dr. Olav Fyske Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni wakati akishirikisha mchango wa mawazo yake kwenye mkutano wa Makanisa Ulimwenguni ulifanyika hivi karibuni kwa kupania kujenga na kuimarisha mshikamano wa dhati na Wakristo wanaoishi huko Mashariki ya Kati, ambao kwa sasa wanakabiliana na hali ngumu ya maisha.

Dr. Tveit amewakumbusha wajumbe wa mkutano huo kwamba, kila Mkristo anapaswa kuubeba vyema Msalaba wake na kumfuasa Kristo, lakini pia kama Jumuiya ya Wafuasi wa Kristo wanachangamotishwa na Mama Kanisa kusaidiana kubebeana Misalaba, kama kielelezo cha upendo na mshikamano wa Wafuasi wa Kristo huko Mashariki ya kati. Mkutano huu ulioanza hapo tarehe 21 hadi tarehe 25 Mei, 2013 ulikuwa umeandaliwa na Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwa kushirikiana na Baraza la Makanisa Mashariki ya Kati. Mkutano huu umefanyika mjini Beirut, huko Lebanon.

Dr. Tveit anasema, mshikamano maana yake ni kuonesha kwamba, kama Wakristo wanathamini zawadi ya maisha, utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu na kwamba, wanapania kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja kwa ajili ya ustawi na mafao ya wengi kwa sasa na kwa siku za usoni. Mshikamano wa Kikristo ni muhimu sana huko Mashariki ya Kati ambayo kwa sasa inakabiliwa na changamoto mbali mbali ikiwa ni pamoja na ukosefu wa haki, amani na autulivu unaopelekea kinzani na migogoro ya kijamii.

Huu ni mwaliko kwa waamini wa dini na madhehebu mbali mbali kufanya kazi kwa pamoja ili kukuza na kudumisha misingi ya haki, amani na maendeleo endelevu. Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwa miaka kadhaa limekuwa likijishughulisha na mchakato unaopania kujenga na kuimarisha misingi ya haki na amani huko Mashariki ya Kati, hususan kati ya Palestina na Israeli.

Baraza la Makanisa kwa kushirikiana na Makanisa mbali mbali huko Mashariki ya Kati linapania pamoja na mambo mengine kudumisha amani pamoja na haki msingi za binadamu; kukomesha uvamizi ili uhuru uweze kutawala na vita kusitishwa.

Ni wajibu na dhamana ya Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, inatoa suluhu ya kisiasa katika mgogoro kati ya Israeli na Palestina. Kushindwa kufanya hivyo, kumepelekea vitendo vya utekaji nyara kuongezeka huko Mashariki ya Kati na kwamba, vita inayoendelea nchini Syria ina madhara makubwa kwa wananchi wasiokuwa na hatia. Mkutano huu umehudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Makanisa huko Mashariki ya Kati.








All the contents on this site are copyrighted ©.