2013-05-29 12:02:45

Parokia ya Laisamis, Jimbo Katoliki la Marsabit, Kenya, inaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu ilipoanzishwa!


Askofu mstaafu Ambrogio Ravasi, Jumapili iliyopita, tarehe 26 Mei 2013 ameongoza umati mkubwa wa waamini na marafiki wa Parokia ya Laisamis, Jimbo Katoliki la Marsabit, Kenya kuadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu ilipofunguliwa, ikiwa ni Parokia ya kwanza Jimboni humo.

Askofu mstaafu Ravasi amewaambia waamini na watu wenye mapenzi mema waliokuwa wamehudhuria katika Ibada hii ya Misa Takatifu kwamba, uwepo wao ni matunda ya imani shirikishi yanayoonesha hija ya Familia ya Mungu nchini Kenya. Hii ni Parokia iliyoanzishwa miezi minne kabla ya Kenya kujipatia uhuru wake kutoka kwa Mwingereza. Parokia hii kwa mara ya kwanza ilihudumiwa na Mapadre Luigi Graiff na Mario Valli kutoka katika Shirika la Wamissionari wa Consolata.

Hii ni Parokia ambayo imedhamiria kujitegemea na kulitegema Jimbo kwa kutumia rasilimali watu na mali inayopatikana Parokiani hapo kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa. Licha ya Parokia hii kufungwa kwa takribani mwaka mmoja na kuendelea kupata huduma kutoka kwa Wamissionari wa Consolata, waamini wameendelea kubaki imara katika imani yao kwa Kristo na Kanisa lake bila kuyumbishwa wala kutetereka, matendo makuu ya Mungu.

Parokia ya Laisamis ina jumla ya vigango vitatu na katika kipindi cha miaka 50 iliyopita imekuwa ni chemchemi ya miito mitakatifu ndani ya Kanisa. Wamissionari wa Consolata walihudumia Parokia hii tangu ilipoanzishwa hadi mwaka 1990 walipoikabidhi kwa Jimbo Katoliki la Marsabit, nchini Kenya.







All the contents on this site are copyrighted ©.