2013-05-29 14:10:33

Kanisa ni familia ya Mungu inayotumwa kutangaza Injili hadi miisho ya dunia!


Baba Mtakatifu Francisko katika katekesi yake, Jumatano, tarehe 29 Mei 2013, baada ya kuhitimisha mfufulizo wa Katekesi kuhusu Kanuni ya Imani, kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ameanza Katekesi Mpya kuhusu Fumbo la Maisha na Utume wa Kanisa, mintarafu Mafundisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican. Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francsiko ameanza kwa kuchambua Kanisa kama Familia ya Mungu.

Kama inavyooneshwa katika mfano wa Baba mwenye huruma, Mwenyezi Mungu anawataka watu wote kuishi na kudumu katika pendo lake ili kuweza kushiriki maisha yake. Kanisa ni sehemu muhimu sana ya Mpango wa Mungu; kwani mwanadamu ameumbwa ili kumfahamu na kumpenda Mwenyezi Mungu licha ya uwepo wa dhambi miongoni mwa wanadamu, lakini Mwenyezi Mungu anaendelea kuwaalika ili waweze kutubu na kumrudia tena.

Baba Mtakatifu anasema, katika utimilifu wa nyakati, Mwenyezi Mungu alimtuma Mwanaye wa Pekee kuja hapa ulimwenguni ili kuanzisha Agano Jipya na la Milele na binadamu wote kwa njia ya sadaka yale pale Msalabani. Kanisa ni tunda la upendo unaopatanisha, kwa njia ya maji na damu iliyobubujika kutoka ubavuni mwa Kristo, pale walipomchoma mkuki ubavuni.

Katika Sherehe ya Pentekoste, Roho Mtakatifu aliwashukia Mitume kwa kuwakirimia nguvu ya kutangaza Injili ya Upendo wa Kristo hadi miisho ya dunia. Baba Mtakatifu anasema, kamwe Kristo hawezi kutenganishwa na Kanisa lake, ambalo ameliwezesha kuwa ni Familia kubwa ya Watoto wa Mungu. Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kuamsha tena ndani mwao ari na moyo wa kulipenda Kanisa, ili kweli liweze kuwa ni Familia ya Mungu, m ahali ambapo kila mtu anajisikia kwamba, anakaribishwa, anaeleweka na kupendwa.

Baba Mtakatifu anaendelea kuwaalika waamini kulipenda na kuliombea Kanisa ili hatimaye, liweze kuwa kweli ni chombo cha huruma, umoja na upendo wa Mungu kwa jirani.

Ni mwaliko pia wa kumwilisha imani kama Familia ya Mungu inayowajibika, kwa kuonesha upendo kwa Familia. Anawaombea Roho Mtakatifu ili awasaidie kutenda mema katika maisha yao ya kila siku. Anawataka waamini kuhakikisha kwamba, Jumuiya zao za Kikristo zinakuwa ni alama ya ukarimu; huruma na upendo wa Mungu kwa jirani.

Anawataka vijana kuwapenda, kuwaheshimu na kuwaombea wazazi wao kwani wao ni chemchemi ya maisha na zawadi kubwa inayowawajibisha mbele ya Mwenyezi Mungu. Anawataka kujitoa kimasomaso kushiriki katika maisha na utume wa Familia: kiroho na kimwili. Anawataka waamini wanaofanya hija ya maisha yao ya kiroho kwenye makaburi ya Mitume, kuimarisha imani yao kwa Kristo na Kanisa lake na kwa namna ya pekee wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Mwaka wa Imani.

Mwishoni, Baba Mtakatifu Francisko, anawaalika waamini na watu wenye mapenzi mema kushiriki pamoja naye katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Ekaristi Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano, kuanzia majira ya Saa Moja Kamili Usiku, Alhamisi, tarehe 30 Mei 2013 na kuhitimishwa kwa Baraka Kuu ya Ekaristi Takatifu kwenye Kanisa la Bikira Maria Mkuu lililoko mjini Roma. Baba Mtakatifu anasema, Ibada ya Ekaristi Takatifu ni kielelezo cha imani na amana muhimu sana katika maisha ya Kanisa na binadamu kwa ujumla wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.