Kanisa linaendelea kuwekeza katika tunu msingi za maisha ya kifamilia!
Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la Familia anasema, Kanisa linaendelea
kuwekeza katika majiundo makini ya tunu msingi za maisha ya kifamilia, ili familia
ziweze kutekeleza dhamana na wajibu wake ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla, kwani
upendo wa binadamu kamwe hauwezi kuwa mkamilifu, unahitaji kuboreshwa siku hadi siku.
Familia ni shule ya upendo, mahali ambapo wanafamilia wanajifunza kuishi kwa
pamoja, wakishirikiana na kushirikishana karama na vipaji walivyokirimiwa na Mwenyezi
Mungu katika hija ya maisha yao. Ni mahali ambapo wanafamilia wanatambua tofauti zao
kuwa ni utajiri mkubwa unawasaidia kujenga na kuimarisha: haki, amani, upendo na mshikamano
ndani ya familia. Wanafamilia wanapaswa kutambua tofauti iliyopo kati yao na kwamba,
utofauti huu si chanzo cha kinzani wala mikingamo, bali ni mwaliko wa kushirikiana
na kukamilishana kadiri ya mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu.
Sayansi
na maadili yawasaidie wanafamilia kutambua wajibu na dhamana yao na kwa namna ya pekee,
wajielekeze kuwaelimisha watoto wao katika maadili na utu wema, kwani kimsingi wazazi
na walezi ndio waalimu wa kwanza wa watoto wao.
Askofu mkuu Jean Laffitte,
Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Familia anabainisha kwamba, uwepo wa wazazi wote
wawili yaani Baba na Mama ni jambo muhimu sana katika makuzi na ukomavu wa watoto.
Wazazi hawa wawili kwa kushirikiana kwa pamoja wanaweza kurithisha tunu msingi za
maisha ya kifamilia, kiutu na kiimani kwa watoto wao na kwamba, dhamana na utume wao
hauna mbadala.
Mama ni kimbilio na usalama wa watoto; Baba kwa upande wake
ni kielelezo cha sheria na utaratibu wa maisha. Lakini wote hawa wanaunganishwa na
kifungo cha upendo na malezi kwa watoto wao, ili waweze kukua na kukomaa na hatimaye,
kufikia utu uzima. Hata hivyo ikumbukwe kwamba, upendo huu bado unasimikwa katika
vionjo vya kibinadamu kumbe, si mkamilifu unapaswa kuboreshwa siku hadi siku. Licha
ya mapungufu haya, anasema Askofu mkuu Jean Laffitte, mtoto anaweza kupata yale mambo
ya msingi.
Semina na Makongamano yanayoendeshwa na Baraza la Kipapa kwenye
Makao yake Makuu kwa wakati huu yanagusia kwa namna ya pekee: dhamana na nafasi ya
wazazi; familia tenge; upendo usiokuwa mkamilifu na wazazi wanapokuwa kinyume cha
matarajio ya watoto wao! Wadau wanaendelea kushirikisha utajiri unaofumbatwa katika
tofauti za maisha ndani ya familia; madhara ya familia tenge na uhusiano na watoto
wao.
Mama Kanisa anatambua na kuthamini Familia kama shule ya utakatifu, haki,
amani, upendo na mshikamano wa kweli, kila mtu anapaswa kutekeleza dhamana na wajibu
wake, ili familia iendelee kupeta, licha ya kinzani na changamoto zinazoendelea kujitokeza
kwa wakati huu.