2013-05-28 07:29:33

Ratiba elekezi kwa Maadhimisho ya Kiliturujia yatakayoendeshwa na Baba Mtakatifu Francisko Mei hadi Julai 2013


Monsinyo Guido Marini, Mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa, hivi karibuni ametoa ratiba elekezi ya Maadhimisho ya Ibada mbali mbali zinazotarajiwa kuongozwa na Baba Mtakatifu Francisko katika kipindi cha Mwezi Mei hadi Julai, 2013. 00:03:46:42

Baba Mtakatifu Francisko baada ya kutembelea na kusali na Familia ya Mungu, Parokia ya Watakatifu Elizabeth na Zakaria, iliyoko mjini Roma alitoa Sakramenti ya Komunio ya kwanza kwa watoto 16 na watu wazima 28, katika Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika Jumapili iliyopita, tarehe 26 Mei 2013. Kanisa pia lilikuwa linaadhimisha Sherehe ya Fumbo la Utatu Mtakatifu. Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kujiandaa kwa matukio mengine ya kikanisa kama ifuatavyo:

Tarehe 30 Mei 2013, Kanisa mjini Vatican linaadhimisha Siku kuu ya Ekaristi Takatifu. Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano lililoko mjini Roma, ambalo kimsingi ni Makao Makuu ya Jimbo kuu la Roma, kuanzia saa 1:00 Usiku na baadaye kufuatiwa na Maandamano makubwa ya Ekaristi Takatifu kupitia mitaa kadhaa ya Mji wa Roma hadi kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria Mkuu.

Hapo waamini watapata nafasi ya kuabudu Ekaristi Takatifu na baadaye, Papa atatoa baraka ya Ekaristi takatifu. Maandamano ya Ekaristi Takatifu kuzunguka mitaa na viunga vya mji wa Roma, waamini wakiwa wameshikilia mishumaa inayowaka imekuwa na mvuto na ushuhuda wa imani kwa Kristo anayefanya hija ya maisha na wafuasi wake hadi utilimifu wa nyakati.

Jumapili, tarehe 2 Juni 2013 kuanzia saa 11:00 hadi saa 12:00 jioni kwa saa za Ulaya, Baba Mtakatifu Francisko ataongoza Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu, akiungana na waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia, watakaokuwa wanaadhimisha Ibada hii kwa wakati huo huo, kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani.

Jumapili, tarehe 16 Juni 2013, Baba Mtakatifu Francisko ataongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kama sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Injili ya Uhai, changamoto kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kusimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya uhai tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi pale Mwenyezi Mungu anapomwita mja wake kutoka katika ulimwengu huu ili kuweza kuungana naye katika maisha ya uzima wa milele.

Jumamosi, tarehe 29 Juni 2013, Kanisa litakuwa linaadhimisha Siku kuu ya Miamba wa Imani: Mitume Petro na Paulo, walioyamimina maisha yao kwa ajili ya kutangaza na kushuhudia imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.

Hii ni siku ambayo Baba Mtakatifu ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa mara ya kwanza na Maaskofu wakuu wapya walioteuliwa hivi karibuni sanjari na kuwavisha Pallio Takatifu; Ibada itakayoadhimishwa kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kuanzia saa 3:30 asubuhi. Pallio takatifu ni alama ya umoja na mshikamano na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Na kwa Ibada hii, Baba Mtakatifu atakuwa anafunga kirago cha Maadhimisho ya Ibada kwa Mwezi Juni 2013.

Jumapili, tarehe 7 Julai 2013, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya Majandokasisi na Wanovisi kutoka katika Seminari na nyumba za malezi. Haya ni Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwa Waseminari na Wanovisi, wanaopaswa kutambua kwamba, Mama Kanisa ana matumaini makubwa kwao kwa sasa na kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo kwa siku za usoni.

Naam, kuanzia Jumatatu tarehe 22 Julai hadi tarehe 29 Julai 2013, Baba Mtakatifu Francisko atakuwa afanya hija yake ya kwanza ya kichungaji nchini Brazil, ili kushiriki na umati wa vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia katika Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani, inayoongozwa na kauli mbiu ”Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa ni wanafunzi”. Injili kama ilivyoandikwa na Mathayo: 28:19.

Kama ilivyo ada, Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican itakula nawe sahani moja ili kuhakikisha kwamba, inakujuvya kwa kina na mapana yale yatakayojiri katika Maadhimisho haya. Ukiwa na haraka zako, unaweza kutembelea katika mtandao wa Radio Vatican kwa anuani ifuatayo:








All the contents on this site are copyrighted ©.