Ondoeni vikwazo na vizingiti vinavyowakwamisha katika kumfuasa Kristo kwenye njia
ya uzima!
Mwenyezi Mungu ndiye Bwana wa nyakati na anawaalika watu wote kumfuasa bila kuweka
masharti wala vizingiti na kwamba, utajiri kisiwe ni kisingizio cha kutoweza kumfuasa
Yesu Kristo kikamilifu kwa kumtolea ushuhuda wa upendo wa dhati, ili hatimaye, kuweza
kurithi maisha ya uzima wa milele. Umwilishaji wa Amri za Mungu ni jambo la muhimu
sana katika maisha ya mwanadamu, lakini mwamini anapaswa kuwa makini zaidi ili kuondokana
na mambo yale ambayo yanaweza kuwa ni kikwazo katika ufuasi wa Kristo.
Ni sehemu
ya mahubiri iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu asubuhi, kwenye Kikanisa
cha Domus Sanctae Marthae kilichoko mjini Vatican. Anasema, kila mtu ana utajiri ambao
amekirimiwa na Mwenyezi Mungu, lakini kwa bahati mbaya, utajiri kama huu umekuwa ni
chanzo cha majonzi na kikwazo cha ufuasi kwa Kristo. Kila mwamini anachangamotishwa
na Kristo kuchunguza dhamiri yake kuona ni kwa jinsi gani ambavyo utajiri wake umekuwa
ni kikwazo cha kumfuasa Kristo katika njia ya uzima wa milele.
Watu wengi
wanataka raha mustarehe pamoja na kuwa na maisha bora; mambo ambayo wakati mwingine
yamekuwa ni kizingiti katika maamuzi ya maisha ya kifamilia, kiasi kwamba, hata watoto
ambao ni zawadi kutoka kwa Mungu wameonekana kuwa ni mzigo usiobebeka na matokeo yake,
watu wengi wanashindwa kujongea kwa Yesu. Baadhi ya watu wanataka mambo mpito! Lakini
Mwenyezi Mungu ana mpango rasmi kwa kila mwanadamu. Huu ni mpango endelevu ambao kamwe
hauwezi kupitwa na nyakati.
Huwezi kumjaribu Kristo anasema Baba Mtakatifu
Francisko kwa kutaka kuwa Padre wa kipindi cha mpito au mwanandoa wa mkataba! Pale
unapokwisha basi, Upadre au ndoa inavunjika. Muda na utajiri ni vikwazo vikuu katika
kumfuasa Yesu. Baba Mtakatifu anawapongeza Wamissionari waliojitosa kimaso maso kuhubiri
Injili ya Kristo sehemu mbali mbali za dunia bila ya kuweka kizingiti katika maisha
na utume wao kwa Kristo na Kanisa lake. Kuna wanandoa ambao pia wameshikamana hadi
pale kifo kilipowatenganisha, huu ndio ufuasi wa Kristo pasi na masharti.
Baba
Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kumwomba Yesu Kristo ili aweze kuwakirimia
ujasiri utakaowafanya kujitosa kimasomaso bila ya woga ili kumfuasa Kristo bila ya
kurudi nyuma. Ibada hii ya Misa Takatifu imehudhuriwa na viongozi na wafanyakazi wa
Baraza la Kipapa la huduma kwa wafanyakazi katika sekta ya afya; wafanyakazi wa Idara
ya Uchumi pamoja na wahudumu wa Zahanati ya Watoto wadogo ya Mtakatifu Martha, iliyoko
mjini Vatican.