2013-05-28 08:16:05

Imarisheni tunu msingi za maisha ya kifamilia ili kukabiliana na changamoto za utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia!


Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la Familia amehitimisha hija ya kichungaji nchini Argentina na Chile ambako alikwenda kuimarisha mchakato unaopania kudumisha tunu msingi za maisha ya familia pamoja na kuishukuru Familia ya Mungu nchini Argentina, kwa kulizawadia Kanisa la kiulimwengu, Baba Mtakatifu Francisko ambaye kwa sasa anaendelea kulipyaisha Kanisa kwa ari na msukumo mpya katika maisha na utume wake.

Akiwa nchini Argentina na Chile, Askofu mkuu Paglia alipata fursa ya kutoa mhadhara kwenye Chuo Kikuu cha Kikatoliki Argentina, kama sehemu ya kumbu kumbu ya Maadhimisho ya Miaka 30 tangu Umoja wa Mataifa ulipotoa Tamko la Haki Msingi za Familia.

Anasema, Familia inakabiliana na matatizo, changamoto na fursa mbali mbali katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Kuna sera na mwelekeo wa kisiasa ambao unataka kufisha na kudhohofisha tunu bora za maisha ya kifamilia mintarafu mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu.

Askofu mkuu Paglia akiwa nchini Argentina amekutana na kuzungumza na familia ambazo hivi karibuni ziliathirika kutokana na mafuriko makubwa. Baraza la Kipapa la Familia, kwa kuguswa na hali hii, liliamua kuunga mkono jitihada zilizokuwa zinafanyika kwa ajili ya kusaidia familia ili ziweze kupata tena mahali pazuri pa kuishi. Ilikuwa ni fursa ya kukutana na kuzungumza na viongozi wa shughuli za kifamilia kutoka Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Amerika ya Kusini.

Askofu Paglia akiwa nchini Chile ambayo waamini wake wengi wana ibada kwa Bikira Maria wa Mlima Karmeli, aliwataka wasomi na wanazuoni nchini humo kuibua mbinu mkakati utakaoiwezesha familia kupewa kipaumbele cha kwanza miongoni mwa vijana wa kizazi kipya. Anasema, kimsingi Familia inafumbatwa katika upendo wa dhati kati ya Bwana na Bibi, kama njia ya kukamilishana, wakiwa tayari kushiriki katika mpango wa kazi ya Uumbaji na malezi kwa watoto wao ambao ni zawadi safi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Askofu mkuu Paglia alipata pia fursa ya kuzungumza na kujadiliana na vijana wa kizazi kipya kuhusu umuhimu wa ndoa na maisha ya kifamilia kadiri ya mpango wa Mungu. Amewataka vijana kusimama kidete na kamwe wasikubali kuyumbishwa na athari za utandawazi zinazotaka kumong'onyoa tunu msingi za kimaadili na utu wema!







All the contents on this site are copyrighted ©.