Papa ajionea mwenyewe maisha na utume wa Parokia zilizoko pembezoni mwa Mji! Atoa
Mahubiri kwa mtindo wa maswali na majibu!
Baba Mtakatifu Francisko kwa mara ya kwanza kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, Jumapili
iliyopita, tarehe 26 Mei 2013 amefanya hija ya kichungaji kwenye Parokia ya Mtakatifu
Elizabeth na Zakaria iliyoko pembezoni mwa Mji wa Roma.
Baba Mtakatifu amefanya
mahubiri yake kwa njia ya maswali na majibu kwa watoto 44 waliopokea Sakramenti ya
Ekaristi Takatifu kwa mara ya kwanza katika maisha yao. Amezungumzia jinsi ambavyo
Bikira Maria akisukumwa na upendo kwa jirani alivyokwenda kwa haraka kumsaidia binadamu
yake Elizabeth aliyekuwa ni mjamzito.
Bikira Maria Mama wa Mungu na Kanisa
yuko daima tayari kuwasaidia wale wote wanaokimbilia ulinzi na maombezi yake; ni alama
ya usalama, imani na matumaini kwa wote wanaomwita. Anawasaidia waamini kuweza kumfahamu
Mwenyezi Mungu aliyejifunua kwa njia ya Yesu Kristo, ili kuyafahamu maisha na kazi
za Fumbo la Utatu Mtakatifu.
Mwenyezi Mungu ni Muumbaji; amegawanyika katika
Nafsi Tatu: Mungu Baba, Mungu Mwana na Mungu Roho Mtakatifu. Mungu Mwana ni Mkombozi
anayewapenda na kuwafundisha wafuasi wake Neno la Mungu. Ndiye aliyeyamimina maisha
yake kwa ajili ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika utumwa wa dhambi na mauti. Mungu
Roho Mtakatifu analitakatifuza Kanisa.
Baba Mtakatifu amewaambia watoto waliopokea
Ekaristi Takatifu kwa mara ya kwanza kwamba, Yesu Kristo katika Fumbo la Ekaristi
Takatifu anawaonjesha upendo wake na kuwakirimia nguvu mioyoni mwao. Anawaongoza na
kuwalinda hadi waweze kuufikia uzima wa milele. Hii ilikuwa ni Katekesi ambayo watoto
waliopokea Komunyo ya kwanza hawataweza kuisahau kwa urahisi katika maisha yao.
Mara
baada ya Misa Takatifu, Papa Francisko amewashukuru waamini wa Parokia ya Mtakatifu
Elizabeth na Zakaria kwa ukarimu waliomwonesha. Amempongeza Padre Alfred, Paroko ambaye
anatimiza miaka 29 ya Ukasisi wake. Amefurahi kuona Parokia ambayo imechangamka na
kuwa na watoto wengi. Amewataka kuendelea kusonga mbele kwa imani na matumaini, daima
wakimkumbuka katika sala zao.