Majadiliano ya kisiasa ni muhimu katika kulinda na kudumisha amani Ukanda wa Maziwa
Makuu
Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania, amependekeza Jumuiya ya Kimataifa ijielekeze
kutafuta suluhu mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) kwa njia ya mazungumzo
badala ya kutegemea ufumbuzi kwa njia ya kijeshi pekee.
Rais Kikwete ametoa
pendekezo hilo Jumapili, Mei 26, 2013, wakati wa mkutano wa kwanza wa Mchakato wa
Kikanda wa Usimamizi wa Amani, Usalama na Ushirikiano katika DRC na Ukanda wa Maziwa
Makuu (ICGRL) uliohudhuriwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), wakuu wa nchi
wanachama wa ICGRL, na viongozi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na
limekubaliwa.
Mkutano huo umefanyika kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Afrika
(AU) mjini Addis Ababa, Ethiopia ambako Rais Kikwete na viongozi wengine wanaohudhuria
Mkutano wa 21 wa Wakuu wa Nchi Wanachama wa AU ambao umefunguliwa Jumapili asubuhi.
Akizungumza
katika mkutano huo, Rais Kikwete amesema kuwa ni jambo zuri na la maana sana kuwa
na Jeshi la Kulinda Amani katika DRC – Force Intervention Brigade – katika Congo chini
ya Umoja wa Mataifa ambako nchi za SADC ikiwamo Tanzania inachangia majeshi lakini
kuwepo kwa jeshi hili mashariki mwa Congo hakutatosha kuleta suluhu ya kudumu nchini
humo.
“Jambo hili tulilofanya ni zuri sana. Tunaendelea na maandalizi ya kupeleka
jeshi mashariki mwa DRC chini ya UN kama ilivyokubaliwa. Tunaamini kuwa katika muda
mfupi, jeshi hili litakuwa la msaada kijeshi, lakini haliwezi kuwa suluhu ya kudumu
kwa tatizo la DRC – majibu ya tatizo hili lazima yawe ya kisiasa,” amesema Rais Kikwete
na kuongeza:
“Nia iwe ni kusikiliza pande zote, kusikiliza malalamiko yote
ya kisiasa kama yapo, malalamiko ambayo ndiyo yanazaa mapambano ya silaha katika
nchi hii jirani. Nia ni kujenga mazingira ya kuelewana na hivyo kuwezesha mazungumzo
kuwa njia muhimu zaidi ya kutafuta mwafaka.”
Kufuatia maelezo yake, Rais Kikwete
amependekeza kuwa katika hatua ya kwanza Jumuiya ya Kimataifa iunge mkono kwa njia
zote mazungumzo yanayoendelea sasa kati ya Serikali ya DRC na waasi wa M23 mjini Kampala,
Uganda ili yaweze kufanikiwa na kuleta maridhiano kati ya pande hizo mbili.
“Haya
ni mazungumzo muhimu sana. Yalitakiwa kuwa ya wiki tatu na sasa yamefikia mwezi wa
sita ni muhimu yaendelea na sote katika Jumuiya ya Kimataifa tuyaunge mkono kwa
sababu tukifanikiwa kupata maelewano kutokana na mazungumzo hayo tutakuwa tumepiga
hatua kubwa.”
Rais Kikwete amesema kuwa aina ya pili ya mazungumzo yanatakiwa
ni kujenga mazingira ambako vikundi vya waasi ambavyo vimejificha katika DRC
na vinaendesha uasi dhidi ya nchi zao za asili – ADF (Uganda) na FDRL (Rwanda)
vinashiriki katika mazungumzo na nchi zao za asili ili kujenga maelewano.
Aina
ya tatu ya mazungumzo, kwa mujibu wa Rais Kikwete, ni yale kati ya Serikali ya DRC
na vikundi vingine vya ndani vya waasi kama vile Mai Mai na vingine. “Hivi viko
vingi na vina malalamiko yao na ni muhimu nayo yasikilizwe na yatafutiwe ufumbuzi
wake.”
Wakati huo huo, Rais Kikwete amekutana na kufanya mazungumzo na viongozi
wawili wa Afrika – Rais Hifikapunye Pohamba wa Namibia na Rais Mohamed Morsy wa
Misri. Katika mazungumzo yao, Rais Kikwete na Rais Pohamba wamezungumzia masuala yanayohusu
SADC wakati mazungumzo kati ya Rais Kikwete na Rais Morsy wamezungumzia masuala yanayohusu
uhusiano kati ya Tanzania na Misri.