2013-05-25 08:40:27

Papa Francisko, Jumapili anatembelea Parokia ya Elizabeth na Zakaria pamoja na kutoa Sakramenti ya Ekaristi Takatifu kwa waamini 44


Katika Maadhimisho ya Fumbo la Utatu Mtakatifu, Papa Francisko, Jumapili tarehe 26 Mei 2013 anatarajiwa kufanya hija ya kichungaji kwenye Parokia ya Watakatifu Elizabeth na Zakaria, iliyoko mjini Roma. Ibada ya Misa Takatifu inatarajiwa kuanza hapo saa 3:30 kwa saa za Ulaya. Katika Ibada hii ya Misa Takatifu, Papa Francisko atato pia Sakramenti ya Ekaristi kwa Wakristo 44. Kati yao kuna watoto 16 na watu wazima 28.

Hii ni hija ya kwanza ya Baba Mtakatifu Francisko kufanya kama Askofu wa Jimbo kuu la Roma tangu alipochaguliwa kuwa ni Khalifa wa Mtakatifu Petro. Hii ni Parokia yenye Wakristo 15,000. Parokia ilianzishwa hapo tarehe 28 Oktoba 1985 kwa hati iliyotolewa na Kardinali Ugo Poletti. Kuanzishwa kwa Parokia hii kulitoa fursa kwa Waamini kuweza kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa kwa heshima zaidi kwani hapo mwanzoni walilazimika kutumia ukumbi kama mahali pa Ibada. Tangu wakati huo, Parokia imeendelea kucharuka katika maendeleo ya watu: kiroho na kimwili.

Tarehe 26 Oktoba 1997, Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alitembelea Parokiani hapo. Ushirikiano kati ya Waamini na Viongozi wao wa Kanisa umefanikisha maendeleo yote yaliyokwisha kupatikana katika Kipindi cha Miaka 25 iliyopita.







All the contents on this site are copyrighted ©.