Hotuba ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete, akifungua warsha ya wazi (open day) kuhusu
mfumo mpya wa ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa miradi ya kitaifa ya kipaumbele,
viwanja vya makumbusho ya taifa, Dar es Salaam, Mei 24, 2013.
Napenda kuchukua
fursa hii kuwakaribisha wote katika Warsha ya Wazi kuhusu mfumo mpya unaoanzishwa
na Serikali wa ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa miradi ya kitaifa ya kipaumbele.
Warsha hii inatoa nafasi ya pekee kwa wananchi kushiriki na kutoa mawazo yao jinsi
ya kuboresha mfumo huo unaopendekezwa. Ni Warsha ya kuelimishana, kubadilishana mawazo
na kufahamishana mipango na mambo ambayo Serikali inatarajia kuyafanya katika siku
za karibuni.
Namshukuru Balozi Ombeni Sefue, Katibu Mkuu Kiongozi, Dkt. Philip
Mpango, Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, viongozi na watumishi wote wa Tume ya
Mipango kwa kuandaa Warsha hii mahsusi. Kwa namna ya pekee nawashukuru pia wataalamu
wa PEMANDU na McKinsey kwa kushirikiana vizuri na wataalam wetu katika kila hatua
ya safari hii ambayo Serikali yetu imeianza.
Ndugu Wananchi;
Kupanga na kutekeleza mipango ya maendeleo sio jambo geni hapa nchini. Ni jambo ambalo
tumelifanya tangu tupate Uhuru na tunaendelea nalo. Serikali ya Awamu ya Kwanza chini
ya Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Nyerere, ilianza na Mpango wa Kwanza wa Maendeleo
mwaka 1961 – 1964. Mpango huo uliainisha maadui watatu wa maendeleo ambao ni umaskini,
ujinga na maradhi. Mikakati mbalimbali na mipango madhubuti ya maendeleo ilibuniwa
ili kupambana na maadui hao. Baada ya hapo ukaja Mpango wa Maendeleo wa Miaka 15
wa mwaka 1964 – 1980, uliokuwa umegawanywa katika vipindi vitatu vya utekelezaji vya
miaka mitano mitano.
Baadhi yenu mtakumbuka kuwa utekelezaji wa vipindi viwili
vya mwanzo ulikuwa wa kuridhisha. Hata hivyo, utekelezaji wa kipindi cha mwisho cha
Mpango ule, yaani kati ya mwaka 1975 – 1980, ulikuwa duni mno. Utekelezaji wake ulivurugwa
sana na changamoto za wakati ule kama vile kupanda sana bei ya mafuta, kuvunjika kwa
Jumuiya ya Afrika Mashariki (1977) na Vita ya Kagera. Mambo haya yalisababisha fedha
zetu nyingi kutumika kuagiza mafuta, kujenga taasisi zetu wenyewe na kutetea mipaka
ya nchi yetu. Rasilimali kidogo tuliyonayo ikaenda huko badala ya kugharamia miradi
ya maendeleo.
Ndugu Wananchi; Pamoja na changamoto zilizojitokeza,
Serikali iliamua kuanzisha mpango mwingine wa maendeleo wa muda mrefu wa mwaka 1981
– 2000. Kwa bahati mbaya mpango huo nao haukutekelezwa kufuatia kuendelea kudorora
kwa uchumi. Kati ya mwaka 1981 na miaka ya 90 mwanzoni, Serikali ilianza kufanya
mabadiliko makubwa ya kiuchumi. Tukawa na National Economic Survival Programme (NESP)
mwaka 1981 – 82 na Structural Adjustment Programme (SAP) mwaka 1982 – 1985. Mipango
hiyo haikutekelezwa vizuri kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ya ukosefu wa rasilimali
za kutosha. Kati ya mwaka 1986 – 89, Serikali kwa kushirikiana na Mfuko wa Fedha
wa Kimataifa (IMF) ikaanza kutekeleza programu ya kwanza ya kufufua uchumi (ERP –
I). Ya pili ikafuatia kati ya mwaka 1989 – 1992.
Mwaka 1994 Serikali ikaanza
kuandaa mpango wa maendeleo wa muda mrefu utaowezesha kuzikabili changamoto mpya kufuatia
mageuzi ya kiuchumi na kijamii yaliyokuwa yanaendelea nchini na duniani kwa ujumla.
Kazi hiyo ilikamilika mwaka 1999 na kuzinduliwa kwa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya
2025. Malengo ya Dira hiyo ni kuleta maendeleo ya haraka nchini na kuifanya Tanzania
kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025. Maana yake ni kwamba wananchi wawe
na chakula cha kutosha, huduma ya elimu na afya iliyo bora iwafikie watu wengi zaidi,
vifo vya watoto na akina mama vipungue, wastani wa kuishi uongezeke, maji safi na
salama yapatikane kwa wote, uhalifu upungue na umaskini uliokithiri usiwepo kabisa
na pato la wastani la Watanzania liwe zaidi ya dola za Kimarekani 3,000. Vile vile
pawe na maendeleo ya viwanda, matumizi ya teknolojia na sayansi yaongezeke, miundombinu
ipanuke na uchumi ukue kwa asilimia 8 au zaidi.
Ndugu Wananchi; Juhudi
kubwa zilizofanywa na Serikali za awamu zote ikiwemo na hii ninayoiongoza mimi zimeleta
mafanikio ya kutia moyo. Kwa mfano, uchumi wa nchi umekua kwa wastani wa asilimia
7 kwa miaka kumi iliyopita, mfumuko wa bei upo chini ya asilimia 10, mapato ya ndani
yameongezeka, mauzo ya nje yameongezeka na hifadhi ya fedha za kigeni imeongezeka
pia. Hata hivyo, idadi ya Watanzania walio maskini bado ni kubwa hususan umaskini
wa kipato. Vile vile bado hatujafanikiwa kufikia malengo katika maeneo mengi tuliyojiwekea.
Hata tathmini ya utekelezaji wa Dira ya Maendeleo 2025 tuliyofanya mwaka 2000 imethibitisha
hivyo. Hatuendi kwa kasi inayotakiwa na utekelezaji wake siyo wa kuridhisha.
Matokeo yake tupo nyuma ya hatua tuliyotakiwa kuwa. Kwa mfano, kwa upande wa safari
ya kuelekea pato la wastani la watu kuwa dola 3,000 mwaka 2025, tulitakuwa tuwe tumefikia
dola 995 mwaka 2010. Lakini ilikuwa tumefikia dola 545 tu. Kwa ukuaji wa uchumi,
tulitakiwa tuwe asilimia 8, lakini tulikuwa asilimia 7.
Zipo changamoto nyingi
za ndani na nje, zilizofanya tusifikie malengo hayo: Kubwa ni misukosuko ya uchumi
wa dunia, uhaba wa rasilimali fedha na ufuatiliaji mdogo katika utekelezaji wa miradi
iliyoainishwa kuleta maendeleo. Aidha, mipango na mikakati ya maendeleo ilikuwa na
vipaumbele vingi kwa wakati mmoja wakati rasilimali za utekelezaji wake ni kidogo.
Hali hii haikutuwezesha kujielekeza ipasavyo kwenye maeneo yenye kuleta matokeo makubwa
na kwa haraka. Ndugu Wananchi;
Baada ya kutafakari yote haya, tukafikiria
namna ya kuweza kufikia malengo yetu ya Dira ndani ya muda uliobakia. Hivyo, tukaamua
kuja na Mpango ya Maendeleo wa Muda Mrefu wa Miaka 15 ambao utatekelezwa katika awamu
tatu za miaka mitano mitano. Katika Mpango wa Kwanza Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/12-2015/16),
maeneo yaliyopewa kipaumbele ni Miundombinu, Kilimo, Viwanda, Huduma za jamii na Uendelezaji
Rasilimali Watu na Utalii, Biashara na Huduma za Fedha.
Changamoto kubwa
ikabaki kuimarisha mfumo wetu wa kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo ili
kuleta matokeo ya haraka. Kuendelea kufanya vilevile tulivyokuwa tukifanya kusingeweza
kuleta mabadiliko tuliyokuwa tunayataka katika utekelezaji wa mipango yetu. Ilibidi
tubadilike, ikiwezekana tukimbie pale ambapo wengine wanatembea. Ndugu Wananchi;
Tukiwa katika hali hiyo ya kutafakari cha kufanya, mwezi Mei, 2011 ikawa bahati
mimi kuhudhuria Mkutano wa Kimataifa wa “Langkawi International Dialogue” uliofanyika
mjini Kuala Lumpur, Malaysia. Katika mkutano huo, Serikali ya Malaysia iliwasilisha
mada jinsi inavyoendesha na kusimamia utendaji wake ikiwemo utekelezaji wa miradi
ya maendeleo na huduma kwa jamii. Mimi na viongozi wenzangu tuliohudhuria mkutano
huo tulivutiwa sana na mfumo wa utendaji wa Malaysia na tukadhamiria kujifunza zaidi
kutoka kwao. Tukaomba watusaidie.
Bahati nzuri Serikali ya Malaysia ikakubali
ombi letu na kuandaa warsha maalum mwezi Novemba, 2011. Ujumbe wa Tanzania kwenye
warsha hiyo ya aina yake uliongozwa na Dkt. Philip Mpango. Waliporudi, tukaamua kuwa
na sisi tuanze kutumia utaratibu wa Malaysia wa “Matokeo Makubwa Sasa” ama kwa Kiingereza
“Big Results Now”.
Ndugu Wananchi; Utekelezaji wa mfumo wa “Big Results
Now” hapa nchini ulianza kwa kuainisha maeneo sita yenye uwezo wa kutupatia matokeo
makubwa kwa haraka. Maeneo hayo ni nishati, elimu, maji, miundombinu, kilimo na utafutaji
fedha. Kazi ya kuchagua maeneo sita ya kwanza nayo haikuwa rahisi. Tulibishana sana
katika kuchagua vipaumbele vichache lakini vyenye kuleta matokeo makubwa. Hatimaye
tukafanikiwa. Vipaumbele hivi vinabeba msingi wa kufungulia fursa za ukuaji uchumi
wa Tanzania kwa ujumla na kuchochea ustawi wa maisha bora kwa wananchi.
Hatua
ya pili ikawa ni kufanya uchambuzi wa kina kupitia awamu ya kwanza ya maabara (lab)
kama alivyoeleza Katibu Mkuu Kiongozi. Kazi hiyo ilitekelezwa kwa wiki sita mfululizo
na wataalam wetu zaidi ya 300 kutoka nyanja na sekta mbalimbali na kukamilika tarehe
05 Aprili, 2013. Nawapongeza sana kwa kazi hiyo kubwa na moyo wao wa kujitolea. Tumeandaa
ratiba ya utekelezaji kwa kila mradi na programu ikionyesha kazi zilizopangwa kufanywa,
mtekelezaji-husika na muda na kukamilisha kazi.
Katika mfumo huu, Mawaziri
na Watendaji katika Wizara na Idara watapimwa kwa vigezo vilivyo wazi na ninyi wananchi
mtapata fursa ya kuvijua vigezo hivi pamoja na matokeo ya upimaji. Hapatakuwa na
siri. Hii itarahisisha usimamizi wa utendaji kwa maana Waziri au Katibu Mkuu atajifunga
yeye mwenyewe kimaandishi na ataweka saini yake kwenye vigezo ambavyo atapimwa navyo
na wananchi mtashuhudia matokeo ya upimaji huo.
Ndugu Wananchi; Ili kuweza
kuratibu vyema shughuli za ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika
mfumo huu mpya, nimeunda chombo maalum kitakachokuwa chini ya Ofisi yangu ambacho
kitajulikana kama President’s Delivery Bureau (PDB). Kazi zake za msingi zitakuwa
ni pamoja na: kupanga na kuendesha shughuli za uchambuzi wa kina wa kimaabara (labs);
kuandaa mikataba ya kupima utendaji kazi wa Mawaziri kwenye miradi na programu za
maendeleo katika wizara zao; kwa kushirikiana na Tume ya Mipango kuishauri Serikali
kuhusu maeneo machache ya kipaumbele yenye kuleta matokeo ya haraka (National Key
Results Areas); kusaidia sekta binafsi kuwekeza kwenye maeneo hayo; na kufanya tathmini
huru ya utendaji kwa viongozi wote hususan Mawaziri katika utekelezaji wa maeneo muhimu
ya kitaifa.
Ndugu Wananchi; Tumefanya kazi kubwa sana ya kuandaa na kuainisha
maeneo ya kimkakati na kuyaandalia programu za kina kwa ajili ya utekelezaji. Lakini
tumeona ni vyema kuwashirikisha wadau na wananchi katika jambo hili kubwa. Ndio maana
tupo hapa kuhakikisha kuwa wananchi kwa ujumla wenu mnapata fursa ya kuchangia katika
miradi na programu hizo kwa maendeleo ya taifa letu na watu wake.
Ndugu Zangu; Sitapenda
kuongea sana hivyo basi nataka niwape nafasi wananchi na wadau wengine mliofika hapa
kupita katika eneo la kila maabara na kupata maelezo ya kina kutoka kwa wataalam.
Muwe huru kuuliza maswali, kujenga hoja, kutoa maoni na kukosoa na kuboresha katika
kila maabara. Baada ya kupata maoni yenu ndipo tutaboresha na kwenda kuyafanyia kazi
maoni na ushauri wenu.
Ndugu Wananchi; Baada ya kusema hayo, napenda
kutamka kuwa Warsha ya Wazi imefunguliwa rasmi. Ninawatakia majadiliano mazuri na
uchangiaji mzuri. Asanteni kwa kunisikiliza