2013-05-23 07:41:07

Wakimbizi kuwezeshwa katika sekta ya elimu ili kukabiliana na changamoto za maisha!


Shirika la kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na Shirika la Wayesuit la Kuhudumia Wakimbizi, hivi karibuni wametiliana sahihi mkataba wa ushirikiano unaopania kuwajengea uwezo wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi kwa kuwapatia elimu ya juu kwa njia ya mtandao katika nchi zile ambazo UNHCR na JRS zinatekeleza majukumu yake. RealAudioMP3

Wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi wanakabiliana na hali ngumu ya maisha, kiasi kwamba, mara nyingi wanajikuta wako pembezoni mwa Jamii. Elimu ni njia makini inayoweza kuwajengea uwezo wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi, ili kuweza kuwajibika barabara katika maboresho ya maisha na Jamii inayowazunguka. Elimu ni njia nyingine inayoweza kutumika pia kuponya madonda ya utengano, chuki na uhsama ndani ya Jamii, kwa kukazia mambo yanayowaunganisha zaidi.

Kuna wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi nchini Yordan, Kenya na Malawi ambao tayari wamekwishajiandikisha kushiriki katika mpango huu wa elimu ya juu kwa njia ya mtandao. Wanafunzi hawa wanasoma kwenye Vyuo Vikuu vya: Regis kilichoko Marekani pamoja na mtandao wa Vyuo vikuu vya Wayesuit vilivyoko nchini Marekani.

Mpango huu unatarajiwa pia kupanuliwa na hivyo kuzishirikisha nchi nyingine kutoka Barani Afrika. Mipango inaendelea huko nchini Chad ili kuwawezesha wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi kutumia fursa ya elimu ya juu kwa njia ya mtandao ili kujiendeleza zaidi.

Elimu ni sehemu ya haki msingi za binadamu na ni kati ya vipaumbele vinavyotolewa na Shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa katika mikakati yake ya maendeleo. Masomo ya elimu ya juu kwa njia ya mtandao yanatarajiwa kwa siku za usoni kuendelea kuhusisha lugha kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Inapania pamoja na mambo mengine kuwajengea uwezo wakimbizi na jumuiya zinazowahifadhi.

Kwa upande wake, Shirika la Wayesuit kwa ajili ya kuwahudumia Wakimbizi linasema, kwa wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi maalum wanaosoma kwenye vyuo vyao vikuu watahudumiwa kwenye eneo hilo na kusaidiwa na Majaalim kutoka katika vitivo wanavyohudumia. Hadi sasa kuna idadi ndogo sana ya wakimbizi na wahamiaji waliobahatika kupata elimu ya juu kwa njia ya mtandao.

Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari yanaiwezesha Jumuiya ya Kimataifa kuwafikishia hata wakimbizi elimu ya juu mahali walipo. Ni matumaini ya viongozi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Wakimbizi kwamba, makubaliano haya yataendelea kuboreshwa zaidi na kuwa ni sehemu ya hali halisi na wala si jambo la kushangaza.

Kunako Mwaka 2012 Shirika la kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa lilizindua mpango mkakati wa miaka mitano unaopania kuongeza kiwango cha idadi ya wakimbizi wanaoshiriki kupata elimu ya juu. Mkataba huu pia unaendelea kuimaarisha ushirikiano kati ya Mashirika ya Umoja wa Mataifa pamoja na Mashirika ya kidini katika kuwahudumia wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi maalum.

Bwana Antònio Guterres, Kamishina mkuu wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi anasema Mashirika ya kidini yana mchango mkubwa katika kukuza na kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini na kiekumene, hali ambayo inasaidia pia kuwalinda wakimbzi na wahamiaji.









All the contents on this site are copyrighted ©.