2013-05-23 11:47:50

vita na machafuko DRC ni tishio la amani, ustawi na maendeleo ya Nchi za Maziwa Makuu!


Machafuko ya kisiasa, kinzani na vita inayoendelea kufuka moshi nchini DRC ni kati ya mambo ambayo yanahatarisha amani, ustawi na maendeleo katika nchi za Maziwa Makuu. Ni maneno ya Bwana Ban Ki-Moon, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa wakati wa ziara yake ya kikazi nchini Msumbiji, DRC na Rwanda, wakati huu, Umoja wa Afrika unapoadhimisha Jubilee ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika.

Vita inayoendelea nchini DRC imekuwa ni sababu ya kuibuka kwa makundi makubwa ya wakimbizi wanaoyahama makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha na mali zao. Katika ziara hii, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa amekagua miradi inayogharimiwa na Umoja wa Mataifa mintarafu utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anabainisha kwamba, licha ya ukata uliosababishwa na myumbo wa uchumi kimataifa, lakini bado Umoja wa Mataifa unapania kuhakikisha kwamba, Malengo ya Maendeleo ya Millenia yanafikiwa. Hii ni pamoja na kutenga asilimia 0.7 ya pato ghafi la taifa kwa ajili ya kusaidia mchakato wa maendeleo.







All the contents on this site are copyrighted ©.