Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania, amelaani vikali fujo na ghasia zilizofanyika
mjini Mtwara, Jumatano, Mei 22, 2013, akisisitiza kuwa raslimali yoyote inayopatikana
katika sehemu yoyote ya nchi yetu ni mali ya Watanzania wote na lazima itumike kuwanufaisha
wote.
Rais anaamini kuwa ni jambo lisilokubalika kuwa raslimali ya nchi inaweza
kuzuiliwa isitoke katika eneo ambako inapatikana kwa vile hakuna nchi yoyote duniani
inayoruhusu jambo la namna hiyo. Nchi hiyo haipo na wala sera za namna hiyo haziwezi
kuanzia Mtwara.
Aidha, Rais anasisitiza kuwa Sera ya Serikali ni kwamba kila
mtu, kila Mtanzania anayo haki ya kunufaika na raslimali ya nchi yetu yakiwemo maeneo
ambako inatoka raslimali. Rais Kikwete haoni sababu yoyote ya msingi ya kufanyika
kwa fujo na ghasia za Mtwara. Fujo hizo hazina kichwa wala miguu, hazina mshiko na
wala waliofanya fujo hizo hawaelezi wanataka nini isipokuwa kuhitimisha nia na dhamira
yao ya kufanya fujo na kuharibu bila sababu mali za wananchi na zile za taasisi za
Serikali.
Itakumbukwa kuwa wakati zilipotokea fujo na ghasia kwa mara ya kwanza
mwanzoni mwa mwaka huu, Waziri Mkuu Mheshimiwa Mizengo Pinda alikwenda Mtwara akakutana
na akazungumza na makundi mbali mbali na wananchi wa Mtwara. Ilionekana kama ulikuwa
umepatikana mwafaka wa kuhakikisha kuwa jambo hilo halitokei tena.
Katika mazungumzo
hayo, Mheshimiwa Pinda aliwaelezea kwa undani kabisa fursa nyingi zinazowasubiri wananchi
wa Mtwara kwa sababu ya ugunduzi wa gesi asilia na mipango ya Serikali kuhakikisha
kuwa Mtwara na maeneo jirani yananufaika. Miongoni mwa mambo mengine, Mheshimiwa Pinda
aliwaeleza yafuatayo: (a). Kwamba kiasi cha viwanda 57 vya shughuli mbali mbali
vitajengwa Mtwara ili kuhudumia shughuli za uzalishaji wa gesi asilia na maendeleo
ya uchumi wa Tanzania kutokana na gesi asilia hiyo. Idadi hii ya viwanda haijapata
kujengwa katika eneo lolote la nchi hii katika historia.
(b). Kwamba kiasi
cha gesi asilia ambacho kitatoka Mtwara kusafirishwa hadi Dar es Salaam kwa shughuli
nyingine za kitaifa ikiwamo kufua umeme ni asilimia 14 tu, na kuwa kiasi kinachobakia
cha asilimia 86 kitabakia Mtwara kwa ajili ya kuzalisha huduma mbali mbali na kuhudumia
idadi hiyo kubwa ya viwanda.
Isitoshe, Rais anajiuliza kuwa kama gesi asilia
isipotoka Mtwara itabakia huko inafanya nini kwa sababu bidhaa yoyote ni lazima ifikishwe
sokoni ili iweze kuuzika. Gesi asilia hiyo ikibakia katika eneo la bahari la Mtwara
itawafaisha vipi wananchi wa Mtwara hata kama wakifanya fujo kila siku?
Rais
Kikwete anawakumbusha wafanya fujo wa Mtwara na vinara wa fujo hizo kuwa Serikali
inao wajibu wa kulinda usalama wa wananchi pamoja na usalama wa mali zao. Hivyo, Rais
Kikwete hakubali fujo na ghasia zilizofanyika Mtwara leo. Anazilaani vikali na wala
hatakubali wafanya fujo wachache kuvuruga amani na usalama wa nchi yetu popote walipo
na kwa kisingizio chochote kile iwe ni kutafuta umarufu wa kisiasa ama kulinda maslahi
binafsi ya kibiashara.
Serikali itawasaka na kuwakamata wote walioshiriki katika
fujo za leo na kuwafikisha mahakamani. Aidha, Serikali itawasaka na kuwakamata viongozi
na vinara wa fujo na ghasia hizo na kuwafikisha mbele ya sheria hata kama wana mapembe
makubwa kiasi gani.
Rais Kikwete anawapa pole sana wananchi wa Mtwara ambao
wameathirika binafsi kwa kuumizwa ama mali zao kuharibiwa katika fujo na ghasia za
leo. Anapenda kuwahakikishia kuwa Serikali yake itachukua hatua za kukomesha vitendo
hivyo vya fujo na ghasia katika eneo hilo.