2013-05-22 08:39:05

Jengeni utamaduni wa majadiliano ya kidini ili kukuza na kuimarisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kweli!


Majadiliano ya kidini ni nyenzo muhimu sana katika kukuza na kudumisha utamaduni wa haki, amani na utulivu. Hii ni changamoto kwa Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo Kanisa linapoendelea kujielekeza zaidi na zaidi katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya sanjari na kudumisha amani na utulivu, mambo msingi katika maendeleo ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Utu na heshima ya binadamu pamoja na mafao ya wengi ni kati ya mambo ambayo kimsingi yanapaswa kuongoza na kutoa dira na mwelekeo wa majadiliano ya kidini na kiekumene miongoni mwa wafuasi wa Kristo. Majadiliano haya yajenge na kuimarisha ushuhuda wa waamini kwa Kristo na Kanisa lake; kwa pamoja wasimamde kidete kupinga utamaduni wa kifo, wakijitahidi kuvumiliana na kuthaminiana, kwani wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Ni changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Askofu Evaristo Chengula wa Jimbo Katoliki Mbeya, Tanzania wakati wa mahubiri yake kwa Waamini wa Kanisa Katoliki kutoka katika Majimbo kumi na nne ya Tanzania, wakati wa hija, kama sehemu ya Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Bikira Maria wa Fatima sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Kwa kipindi cha siku tatu, mahujaji hao wamesali na kulitafakari Neno la Mungu ambalo kimsingi linapaswa kuwa ni taa na dira inayoongoza maisha yao ya kila siku.

Askofu Chengula anawaalika Wakristo kujenga na kudumisha fadhila ya huruma, upendo na unyenyekevu; daima wakipania kushirikiana na waamini wa dini na madhehebu mengine bila kuwasahau watu wenye mapenzi mema kwa ajili ya maendeleo na ustawi wa wananchi wa Tanzania katika ujumla wao. Migogoro na kinzani za kidini au kisiasa ni vikwazo vikubwa kwa maendeleo ya mwanadamu.

Askofu Chengula afafanua kwamba, kukosa na kukosehana ni sehemu ya ubinadamu, lakini kusamehe na kusahau ni mwanzo wa njia ya utakatifu wa maisha. Msamaha na haki ni fadhila muhimu sana katika ujenzi wa mshikamano wa upendo miongoni mwa Jamii. Waamini wajitahidi kumtanguliza Mwenyezi Mungu katika maisha na vipaumbele vyao, pamoja na kumheshimu binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu ni kielelezo makini cha fadhila za Kikristo, lakini zaidi katika: kuhudumiana, kusaidiana na kuendeleza zawadi ya maisha kwa njia ya kufanya kazi kwa juhudi, bidii na maarifa. Familia Takatifu iwe ni kioo cha tunu bora za maisha ya kifamilia miongoni mwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema. Familia zijifunze kusali, kutafakari Neno la Mungu pamoja na kulimwilisha kwa njia ya matendo ya huruma, kama kielelezo cha imani tendaji, hasa wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Mwaka wa Imani.

Wanafamilia wajitahidi kutoa malezi bora kwa watoto wao na wao wenyewe wakionesha kuwa ni mfano wa kuigwa na Jamii inayowazunguka. Wawe imara kutekeleza wajibu na dhamana yao ndani ya Familia na Jamii katika ujumla wake, kwani kimsingi Familia inapaswa kuwa ni chimbuko la imani, matumaini na mapendo ya Kikristo.

Kila mwamini kutokana na dhamana aliyojitwalia wakati wa Ubatizo na kuimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara anashiriki ukuhani, unabii na ufalme wa Kristo katika hija ya maisha yake hapa duniani. Waamini wajitahidi kulijenga na kulitegemeza Kanisa la Kristo kwa hali na mali.

Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kufunga hija ya mahujaji kutoka mikoa kadhaa ya Tanzania imehudhuriwa pia na Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki la Morogoro.







All the contents on this site are copyrighted ©.