2013-05-22 07:50:12

Hali ya hatari inapaswa kwenda sanjari na ushiriki wa wanasiasa katika kulinda na kudumisha: haki, amani na utulivu nchini Nigeria


Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria baada ya tafakari na upembuzi yakinifu linasema kwa sasa linaunga mkono jitihada za Serikali ya Nigeria ya kupambana na Kikundi cha Boko Haram Kaskazini mwa Nigeria kwa Serikali kutangaza hali ya hatari, kama sehemu ya mkakati wa kudhibiti kikundi hiki ambacho kimekuwa ni chanzo kikuu cha maafa na madhulumu ya kidini nchini Nigeria.

Hayo yamebainishwa na Askofu mkuu Ignatius Ayau Kaigama, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria wakati akizungumza na waandishi wa habari hapo tarehe 21 Mei 2013. Ni matumaini ya Maaskofu kwamba, hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Nigeria ni kwa ajili ya mafao ya wananchi wa Nigeria katika ujumla wao. Hii ni changamoto ya kuhakikisha kwamba, taifa linatumia rasilimali na fursa zilizopo ili kutatua mgogoro huu ambao umekuwa ni kikwazo kikubwa cha maendeleo ya wananchi wa Nigeria.

Wakati Serikali inaendelea kuimarisha juhudi zake kwa njia ya vikosi vya ulinzi na usalama, lakini wanasiasa pia hawana budi kushiriki kikamilifu katika mchakato huu unaopania kulinda na kudumisha haki, amani na utulivu nchini Nigeria. Uchaguzi mkuu nchini humo kisiwe ni kisingizio cha kushindwa kudhibiti vitendo hivi kwa kuogopa kunywima kura na watu wanaounga mkono kikundi cha Boko Haram.







All the contents on this site are copyrighted ©.