2013-05-21 09:20:38

Benki ya Vatican kuendelea kuimarisha misingi ya ukweli na uwazi katika utekelezaji wa majukumu yake!


Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni amewaambia Mabalozi waliowasilisha hati zao za utambulisho kwamba, fedha inapaswa kutumika katika mchakato wa kuwaletea watu maendeleo na kamwe isiwe ni chambo cha kutaka kuwatala wa kuwagandamiza watu. Ukweli, uwazi na maadili ni kati ya mambo ambayo yanapaswa kupewa msukumo wa pekee katika masuala ya fedha na uwekezaji. Hii ndiyo changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, inayoendelea kuvaliwa njuga na Papa Francisko kwa sasa.

Kwa kuzingatia mantiki hii, Rais wa Benki ya Vatican bwana Ernst Von Freyber, katika mahojiano maalum na Radio Vatican alibainisha kwamba, Benki ya Vatican, kabla ya kufunga mwaka 2013, inatarajia kufungua tovuti yake itakaotumika kuonesha shughuli mbali mbali zinazotekelezwa na Benki ya Vatican katika masuala ya fedha pamoja na kutoa taarifa yake ya Mwaka itakayoonesha shughuli mbali mbali za Benki ya Vatican.

Uongozi wa Benki ya Vatican unaendelea kuimarisha ushirikiano pamoja na kupokea ushauri na vigezo vya kimataifa katika kupambana na utakatishaji wa fedha haramu zinazoweza kutumiwa pia kugharimia vitendo vya kigaidi sehemu mbali mbali za dunia. Ni pale tu ambapo thamani za jamii na kutete roho ya upendo, kutoa kwa moyo radhi, mshikamano, ustahilivu na haki vitakapotawala hapo ndipo jamii itakapoweza kujenga hali ya mazingira sahihi kwa matumizi sahihi ya fedha kwa mafao ya wengi.

Jamii inakumbushwa kwamba, fedha ina nguvu ya kuokoa, kukomboa, kujenga na kuimarisha upendo sanjari na kusaidia jitihada za kukuza na kuimarisha utu wa mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Lakini fedha pia ina nguvu ya kumfanya mwanadamu kuwa mtumwa na pamoja na kuibua hisia ya kupenda kuwatala wengine; kunyonya na kuwa na matumizi mabaya ya fedha. Fedha itumike kwa uwajibikaji mkubwa.







All the contents on this site are copyrighted ©.