Mzee Ali Abdallah Kleist Sykes muasisi wa TANU afariki dunia mjini Nairobi
Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania amepokea kwa majonzi makubwa taarifa za kifo
cha Mzee Ali Abdallah Kleist Sykes, mmoja wa waanzilishi 17 wa Chama cha Tanganyika
African National Union (TANU) na mpigania maarufu wa uhuru wa Tanganyika, ambaye ameaga
dunia Jumapili, Mei 19, 2013. Mzee Ali Sykes ambaye alikuwa anashikilia kadi nambari
mbili ya Chama cha TANU amefariki dunia majira ya saa saba kwenye Hospitali ya Agakhan
mjini Nairobi, Kenya ambako alilazwa wiki mbili zilizopita kwa matatizo ya ugonjwa
wa moyo.
Katika salamu zake kwa Balozi Abbas Sykes, mdogo wake marehemu Ali
Sykes, Rais Kikwete amesema: “Nimepokea kwa majonzi makubwa taarifa za kifo cha Mzee
wetu Ali Abdallah Kleist Sykes ambaye nimejulishwa kuwa amepoteza maisha yake kiasi
cha saa saba mchana siku ya Jumapili, kwenye Hospitali ya Agakhan mjini Nairobi, Kenya.”
Amesema
Rais Kikwete: “Mzee Ali Sykes ametoa mchango usiokuwa na kifani na usioweza kupimika
katika historia ya kupigania Uhuru wa Tanganyika na hatimaye kupatikana kwa uhuru
wa nchi yetu. Haikuwa kazi rahisi kupambana na Wakoloni na bila ya uthubutu wake na
wenzake pengine historia ya nchi yetu ingekuwa tofauti na ilivyo sasa.”
Ameongeza
Rais Kikwete: “Hata baada ya kupatikana kwa Uhuru wa Tanganyika, Mzee Ali Abdallah
Kleist Sykes aliendelea kutoa mchango wa manufaa kabisa kuhusu jinsi ya kuendesha
nchi yetu. Ametutoka wakati tunahitaji sana ushauri, hekima na busara zake.”
“Nakutumia
wewe Mzee Abbas Abdallah Kleist Sykes salamu zangu za rambirambi kufuatia msiba huu
mkubwa. Aidha, kupitia kwako naipa familia nzima pole nyingi kwa pigo hili la kuondokewa
na mmoja wa nguzo kuu za familia na Uhuru wa nchi yetu. Ameifanyia nchi yetu mambo
mengi na tutaendelea kumkumbuka na kumuzeni kwa yote aliyotufanyia na kutuachia,”
amesema Rais kikwete na kuongeza:
“Napenda mjue kuwa niko nanyi katika msiba
huu mkubwa. Najiunga nanyi katika kuombleza kifo cha Mzee wetu na kiongozi wetu. Naelewa
majonzi na machungu yenu na namwomba Mwenyezi Mungu awape nguvu na subira ya kuhimili
kishindo cha msiba huu. Aidha, naungana nanyi katika kumwomba Mwenyezi Mungu aiweke
peponi roho ya Marehemu Mzee Ali Abdallah Kleist Sykes. Amin.”