2013-05-19 09:47:58

Wanachama wa vyama na mashirika ya kitume waadhimisha Mwaka wa Imani mjini Vatican


Kesha la Maadhimisho ya Siku kuu ya Pentekoste kwa mwaka 2013 limekwenda sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwa kuwashirikisha wanachama wa vyama na mashirika ya kitume 150, kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Wanachama hawa waliianza siku ya Jumamosi kwa kutembelea kaburi la Mtakatifu Petro pamoja na kukiri imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, changamoto ya kuendelea kutolea ushuhuda imani hiyo katika uhalisia wa maisha.

Kesha la Pentekoste limekuwa ni fursa kwa waamini: kusali na kufanya tafakari ya kina kuhusu Neno la Mungu ambalo limekuwa ni taa na dira inayowaongoza waamini katika hija ya maisha yao hapa duniani wakiungana na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Uwepo wa umati mkubwa wa waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia ni ushuhuda wa imani tendaji na changamoto iliyotolewa na Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.

Ni maneno ya Askofu mkuu Rino Fisichella, wakati alipokuwa anamkaribisha Baba Mtakatifu Francisko ili kuungana na umati mkubwa wa waamini waliokuwa wamemiminika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro na viunga vyake kwa ajili ya kuadhimisha Mwaka wa Imani, wakitoa ushuhuda wa yale yaliyojiri siku ile walipokutana na Yesu Kristo Mfufuka kwa mara ya kwanza. Zote hizi ni karama za Roho Mtakatifu ambazo amelijalia Kanisa katika kipindi cha miaka 50 iliyopita.

Ni wanachama wa vyama na mashirika ya kitume yenye karama na mapaji mbali mbali walioamua kuyatumia kwa kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Uinjilishaji kwa ulimwengu mamboleo. Ni waamini wenye ari, uvumilivu na ujasiri uliowafanya kuweza kuungana na waamini wengine kutoka sehemu mbali mbali za dunia ili kushirikishana utajiri wa Neno la Mungu na ushuhuda wa imani tendaji.

Wote hawa anasema Askofu mkuu Fisichella wako tayari kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia. Wanatambua changamoto na magumu wanayokutana nayo katika maisha na utume wao, lakini kamwe hawezi kukata tamaa, kwani wamekirimiwa nguvu ya Roho Mtakatifu.








All the contents on this site are copyrighted ©.