"Nimeng'atuka kwa ajili ya mafao na ustawi wa Familia ya Mungu Jimbo kuu la Songea"
Baba Mtakatifu Francisko, hivi karibuni aliridhia Ombi lililotolewa na Askofu mkuu
Norbert Wendelin Mtega wa Jimbo kuu la Songea, Tanzania kutaka kung'atuka kutoka madarakani.
Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania likafafanua kwamba, hii ni kutokana na sababu
za afya ambazo zimemsukuma Askofu mkuu Mtega kung'atuka kutoka madarakani.
Hivi
karibuni, Askofu mkuu mstaafu Mtega alizungumza na waandishi wa habari akikazia kwamba,
ameamua kung'atuka kutoka madarakani kutokana na sababu za afya kuanza kuleta mgogoro
na hivyo kumnyima fursa ya kuweza kuwahudumia kwa ukamilifu waamini wa Jimbo kuu la
Songea. Anasema, amekuwa akisumbuliwa na magonjwa mbali mbali, ikiwa ni pamoja na
shinikizo la damu, miguu na magoti kujaa maji, kukosa usingizi kwa muda mrefu na hali
ya kusikia kizungu zungu, jambo ambalo limempekea kuanguka mara kadhaa.
Anasema
hizi ni dalili za hatari na kwamba, haya yalikuwa ni matatizo makubwa ya afya ambayo
yanamnyima fursa ya kutekeleza wajibu wake barabara wa kuongoza, kufundisha na kuwatakatifuza
watu wa Mungu, Jimbo kuu la Songea. Kutokana na sababu hizi msingi kwa hiyari na utashi
wake kamili akaamua kumwomba Baba Mtakatifu Francisko aliangalie jambo hili pamoja
na kumpatia nafasi ya kumtafuta Askofu mkuu mwingine atakayeendeleza kazi ya Kristo,
Jimbo kuu la Songea. hakupenda kung'ang'ania madarakani kwani hasara zake zingekuwa
kubwa kwa Familia ya Mungu Jimbo kuu la Songea.
Anaendelea kumwomba Mwenyezi
Mungu amjalie afya na maisha ili aendelee kuchangia katika ustawi na maendeleo ya
watanzania hata katika awamu hii ya maisha yake. Amewataka watanzania kushikamana
kwa dhati ili kujenga na kudumisha umoja, upendo, haki na amani bila kuendekeza ukabila
na udini, mambo ambayo kimsingi ni sumu ya maendeleo ya binadamu.
Anasema,
Kanisa bado linakabiliwa na changamoto ya kuwaendeleza watanzania katika nyanja mbali
mbali za maisha, lakini zaidi katika sekta ya elimu, afya, maji na utunzaji bora wa
mazingira. Kanisa halina budi kuendeleza mchakato wa kujitegemea na kuwategemeza waamini
wake.
Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu Norbert Wendelin Mtega amekuwa ni Askofu
kwa kipindi cha miaka 28, kati ya miaka hii, ametumia miaka 6 kuliongoza Jimbo Katoliki
la Iringa na miaka 22 amekuwa ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Songea. Kwa miaka mingi
amekuwa ni Mwenyekiti wa Idara ya Elimu Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania na mafanikio
yake yanaonekana kwa kuzaliwa kwa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino cha Tanzania
kinachoendelea kutamba kwa huduma na ubora wa elimu nchini Tanzania.
Askofu
mkuu mstaafu Norebert Mtega ameshiriki mara kadhaa katika Maadhimisho ya Sinodi za
Maaskofu na mara ya mwisho alichaguliwa kuwa ni kati ya Wajumbe wa Sekretarieti ya
Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika.