2013-05-19 15:02:55

Kanisa linasali kwa ajili ya Familia ya Mungu duniani


Maadhimisho ya Sherehe ya Pentekoste kwa Mwaka 2013 yameongozwa na kauli mbiu “Mimi nina amini niongezee imani” . Waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia walishiriki pia katika Sala za Waamini, ambazo kwa namna ya pekee, waamini wamemwomba Roho Mtakatifu ili aweze kulidumisha Kanisa katika umoja unaobubujika kutoka katika Sadaka ya Kristo Msalabani na umoja huu uweze kuenea miongoni mwa watu wa Mataifa. RealAudioMP3

Pentekoste ni Siku kuu ya Waamini walei na Kanisa limewaombea wanachama wa vyama na mashirika ya kitume ili kwa kusaidiwa na Roho Mtakatifu waoneshe ile sura ya Kristo pamoja na kuwakirimia uwezo wa kushuhudia imani yao kwa nguvu na upendo unaokoa.

Kanisa linatambua kwamba, bado kuna wadhambi, wenye mashaka na wasioamini. Wote hawa wameombewa ili Roho Mtakatifu aweze kuifungua mioyo yao kusikiliza na kuitii Injili inayowawezesha kumfahamu Bwana Yesu Kristo.

Mama Kanisa anawajali na kuwathamini vijana wa kizazi kipya. Hawa wameombewa ili waweze kuwa waaminifu katika urafiki wao na Yesu Kristo anaye wachangamotisha kuchuchumilia utakatifu wa maisha. Roho Mtakatifu awawezeshe kufanya maamuzi ya kishujaa.

Mwishoni, Kanisa limesali na kumwomba Roho Mtakatifu awaangazie viongozi wa Serikali na watu wenye mapenzi mema, ili macho yao yaone mahitaji msingi ya ndugu zao, hatimaye waweze kujielekeza kufanya maamuzi bora kwa mafao ya wengi, haki na amani. Sala kwa lugha ya Kiswahili imetolewa na Dr. James Msekela, Balozi wa Tanzania nchini Italia.

Itakumbukwa kwamba, waamini wanaoshiriki katika Ibada ya Misa Takatifu kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro wanaweza kupata Rehema Kamili, ikiwa kama watafuata masharti yaliyowekwa na Mama Kanisa. Yaani, kutokuwa na doa la dhambi ya mauti au dhambi ndogo. Kupokea Sakramenti ya Kitubio na Ekaristi Takatifu pamoja na kusali kwa nia za Baba Mtakatifu Francisko.








All the contents on this site are copyrighted ©.