2013-05-18 10:51:32

Mapadre na Watawa hawaruhusiwi kujihusisha na masuala ya kisiasa!


Baraza la Maaskofu Katoliki DRC limetoa mwongozo unaowakataza Mapadre na Watawa kugombea nafasi za uongozi kwenye Tume ya Huru ya Uchaguzi nchini DRC. Tume hii ina wajibu wa kuratibu mchakato wote wa uchaguzi kuwa unafanyika katika haki na uhuru kamili. Kwa sasa vyama mbali mbali vya kisiasa na vile vya kiraia vinajipanga kuhakikisha kwamba, vinakuwa na uwakilishi katika Tume Huru ya Uchaguzi nchini DRC kadiri ya sheria iliyotungwa na kupitishwa na Bunge hivi karibuni.

Padre Fèlicien Mwanama, Katibu mkuu msaidizi wa Baraza la Maaskofu Katoliki Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo anasema, kadiri ya sheria za Kanisa Mapadre na Watawa hawaruhusiwi kujihusisha na masuala ya kisiasa. Sheria zinafafanua kwamba, Askofu mahalia anaweza kutoa kibali kwa Padre au Mtawa kujiunga na shughuli za kisiasa kwa sababu maalum.

Tume Huru ya Uchaguzi DRC itaundwa na kundi la watu kumi na tatu: sita watachaguliwa kutoka katika Chama Tawala na wajumbe wanne watachaguliwa kutoka katika vyama vya upinzani na watatu, hawa watachaguliwa kutoka katika vyama vya kiraia. Katiba ya DRC inaonesha kwamba, Tume hii itakuwa chini ya Mwenyekiti na wengine ni wajumbe watakaoshiriki katika utekelezaji wa shughuli na maamuzi ya kila siku na kwamba, inatakiwa kutekeleza majukumu yake bila kuingiliwa na wanasiasa wala Serikali.

Hivi karibuni, Baraza la Maaskofu DRC liliitaka Serikali na vyama vya kisiasa nchini humo kuanzisha mchakato wa majadiliano ya kitaifa unaopania kuponya madonda ya kinzani na utengano; mambo ambayo yamechangia kukosekana kwa amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa. Rasilimali na utajiri wa nchi utumike kwa mafao ya wengi badala ya kuendelea kuwanufaisha wajanja wachache ndani ya Jamii. Kuna haja pia ya kuleta mabadiliko katika sekta ya kilimo kwa kuondokana na kilimo cha jembe la mkono, ili kuongeza tija na pato kwa wakulima hasa wale wanaoishi vijijini.

Baraza la Maaskofu Katoliki DRC linasikitishwa na hali ya umaskini wa hali na kipato unaowakumba wananchi wengi kwa sasa. Ili haki, amani na utulivu viweze kupatikana na kudumishwa, kuna haja ya kufanya mageuzi makubwa katika: Mahakama na Jeshi la Polisi na pamoja na Vikosi vya Ulinzi na Usalama; kama dawa ya kupambana na ufisadi, rushwa na ubadhirifu wa mali ya umma; mambo ambayo pia yamechangia kuporomoka kwa amani nchini DRC.







All the contents on this site are copyrighted ©.