2013-05-18 13:27:48

Bi Angela Merkel akutana na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, tarehe 18 Mei 2013 amekutana na kuzungumza na Chancellor wa Shirikisho la Ujerumani Bi Angela Merkel. Baadaye, alikutana na kuzungumza na Askofu mkuu Domique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa.

Katika mazungumzo kati ya Baba Mtakatifu Francisko na Bi Angela Merkel, wamegusia uhusiano uliopo kati ya Ujerumani na Vatican. Wamepembua hali ya: kijamii, kiuchumi, kisiasa na kidini Barani Ulaya na duniani katika ujumla wake. Viongozi hao wamekazia kwa namna ya pekee, umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu. Kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kukomesha vitendo vya madhulumu dhidi ya wakristo kwa kukazia uhuru wa kidini pamoja na ushirikiano wa kimataifa unaopania kujenga na kudumisha amani.

Viongozi hawa wameangalia pia tunu msingi za maisha ya Jumuiya ya Ulaya, uwajibikaji duniani kwa kusema kwamba, kuna haja ya kwa viongozi wa Serikali na Kidini kutekeleza wajibu wao kama kikolezo cha maendeleo endelevu yanayojengeka katika msingi wa utu, heshima ya binadamu pamoja na mshikamano unaoongozwa na kanuni ya auni.







All the contents on this site are copyrighted ©.