2013-05-18 08:58:56

Barua ya wazi kutoka SECAM kuhusu Ukwepaji wa kodi


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM limeandika barua ya wazi kwa wajumbe wa Mkutano wa Kodi Barani Ulaya utakaofanyika hapo tarehe 22 Mei 2013 kuangalia uwezekano wa kuwa na sera na sheria makini zitakazowabana wakwepa kodi wanaokwamisha juhudi za watu kujiletea maendeleo yao wenyewe.

Hili ni kundi ambalo limeendelea kujinufaisha kwa kujipatia pato kubwa lisilo halali kutokana na kukwepa kulipa kodi katika nchi husika, lakini hali ni mbaya zaidi kwa nchi maskini duniani.

Askofu Gabriel Mbilingi, Makamu wa Rais, SECAM anasema, wamepokea kwa mikono miwili uamuzi uliofanywa na Umoja wa Ulaya wa kuitisha mkutano wa Kodi Barani Ulaya, juhudi ambazo zinapaswa kwenda sanjari na utashi wa kisiasa wa kutekeleza maamuzi magumu kwa ajili ya mafao ya Jamii husika. Kila mwaka kuna mammillioni ya fedha yanatoweka, kwa njia ya kukwepa kulipa kodi na matokeo yake Serikali zinakosa mapato au zinapata "kiduchu" ikilinganishwa na kodi halali iliyopaswa kutolewa.

Takwimu za kuaminika kutoka katika taasisi za Fedha Kimataifa, "Global Financial Instutions" zinaonesha kwamba, kila mwaka Dolla za Kimarekani millioni 725 hadi millioni 810 zinatoroshwa kutoka katika nchi maskini zaidi duniani. Kiasi hiki cha fedha ni kikubwa kwani kinahitajika kwa ajili ya kuwekeza katika maboresho ya hali ya maisha ya wananchi wanaoishi katika Nchi zinazoendelea. Ukwepaji wa kodi ni ukiukwaji wa haki, jambo ambalo halina budi kufanyiwa marekebisho ya haraka na taasisi za fedha kimataifa na kitaifa.

Askofu mkuu Mbilingi anawaambia wajumbe wa mkutano wa kodi Barani Ulaya kutambua kwamba, wanayo dhamana nyeti ya kimaadili na kisiasa kufanya mabadiliko haya yanayohitajika kwa sasa, ili kujenga na kuimarisha mshikamano wa kidugu kwa kupunguza anasa, ili fedha hizi zisaidie katika mchakato wa kuwaletea wananchi maendeleo endelevu pamoja na kuenzi amani na utulivu. Ni matumaini ya SECAM kwamba, Bwana Herman Van Rompuy, Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya, watalishughulikia tatizo hili kwa uwajibikaji utakaojionesha katika matendo kwa nchi za Ulaya na katika Jumuiya ya Kimataifa.

SECAM inashauri kwamba, kuwepo na viwango vya kimataifa kuhusiana na ubadilishanaji wa habari na takwimu za fedha katika hali ya uwazi ili mamlaka za kodi na mapato ziweze kutoza kodi stahiki. Kuna haja ya kuendelea kufanya maboresho kwa kuzingatia ukweli na uwazi katika masuala ya fedha kimataifa na kitaifa ili kuwawajibisha wahusika katika masuala ya kodi.

Makampuni ya kimataifa hayana budi kutekeleza mitaji yake kwa kuzingatia ukweli na uwazi. Sheria zilizopo ziimarishwe na kuborshwa ili kuwabana wakwepa kodi na kwamba, kila upande unapaswa kutekeleza wajibu wake kwa njia ya haki pamoja na kutafuta mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.