Vyombo vya habari vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa viwe mstari wa mbele kulinda
na kutetea tunu msingi za maisha ya familia!
Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari yasaidie kuenzi na kudumisha tunu bora
za maisha ya familia, dhamana inayoendelezwa na Mama Kanisa katika maisha na utume
wake. Hii ni changamoto inayopaswa kufanyiwa kazi na waandishi wa habari nchini Kenya.
Ni ujumbe uliotolewa na Askofu Martini Kivuva wa Jimbo Katoliki la Machakosi
ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Mawasiliano ya Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya,
katika Maadhimisho ya Siku ya 47 ya Mawasiliano Ulimwenguni sanjari na kumbu kumbu
ya miaka kumi tangu Radio Waamini inayoendeshwa na kumilikiwa na Baraza la Maaskofu
Katoliki Kenya ilipoanzishwa.
Askofu Kivuva anawataka waandishi wa habari
na watumiaji wa mitandao ya kijamii kusaidia jitihada za kuendeleza tunu msingi za
maisha ya kifamilia. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, Familia kwa sasa ni taasisi
inayokabiliwa na changamoto nyingi, jambo ambalo Kanisa linapaswa kulisimamia kidete.
Vyombo vya habari vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa viwe mstari wa mbele
kutetea na kulinda tunu msingi za maisha ya kifamilia. Wazazi na walezi kwa upande
wao wanachangamotishwa pia kutekeleza majukumu yao kikamilifu kwa kutambua haki na
wajibu wao