2013-05-17 08:13:46

Ujumbe wa Sherehe ya Pentekoste kwa Mwaka 2013 kutoka kwa Baraza la Makanisa Ulimwenguni


Basi yeye, akiisha kupandishwa hata mkono wa kuume wa Mungu, na kupokea kwa Baba ile ahadi ya Roho Mtakatifu, amekimwaga kitu hiki mnachokiona sasa na kukisia. Ni sehemu ya Neno la Mungu kutoka katika Kitabu cha Matendo ya Mitume ambayo ni kauli mbiu inayoongoza ujumbe wa Siku kuu ya Pentekoste kutoka kwa Marais wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwa mwaka 2013. RealAudioMP3

Katika kipindi cha Pasaka, waamini wamepata fursa ya kusherehekea ufufuko na hatimaye, kupaa kwa Bwana Yesu Kristo mbinguni. Kanisa kwa sasa linaadhimisha Sherehe ya Pentekoste, siku ile ambayo Mwenyezi Mungu aliukirimia ulimwengu zawadi ya Roho Mtakatifu, changamoto kwa waamini kumwongokea Mwenyezi Mungu kwa njia ya Yesu Kristo sanjari na kuwatumikia jirani zao ambao bado hawajabahatika kusikia Habari Njema ya Wokovu ikitangazwa masikioni mwao kwamba, kwa hakika Yesu anawapenda.

Itakumbukwa kwamba, hata kabla ya Wakristo wa kwanza kuadhimisha Sherehe hii, Wayahudi walikuwa wanaisherehekea kwa kama Siku kuu ya Mavuno, kwa kumtolea Mwenyezi Mungu mavuno ya kwanza. Walikumbuka jinsi ambavyo Mwenyezi Mungu alivyowakomboa kutoka utumwani Misri pamoja na kuwapatia Amri kumi, dira na utambulisho wao kama taifa teule la Mungu. Miaka mingi imekwisha yoyoma tangu Waisraeli walipoadhimisha Sherehe ya Pentekoste, wakikumbuka kazi ya ukombozi iliyotekelezwa na Mwenyezi Mungu.

Leo hii Pentekoste imepata sura na maana mpya. Waamini hawalazimiki tena kumtolea Mwenyezi Mungu mavuno ya kwanza na kinyume chake ni kwamba, Mwenyezi Mungu anawakirimia waamini zawadi ya Roho Mtakatifu anayewasha mioyo ya waamini kwa upendo wa Kimungu kwa kuonesha kutoka kwa Kristo Mfufuka wokovu wa ulimwengu.

Katika miaka ya hivi karibuni watu wengi wameendelea kukabiliana na changamoto mbali mbali: kifedha na kiroho hali inayotishia amani na usalama wa dunia. Ujio wa Roho Mtakatifu uamshe tena moyo n aari ya kiekumene, ili waamini waweze kujikita kutafuta umoja na mshikamano miongoni mwa wafuasi wa Kristo. Waamini na watu wote wenye mapenzi mema washikamane kwa njia ya sala, kwa kujikatalia ili kutenda haki na kutembea katika njia ya Mungu. Hivi ndivyo Baraza la Makanisa kutoka Pacific limetafakari wakati wa Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 tangu Baraza hili lilipoanzishwa kutoka Pacific.

Marais wa Mabaraza ya Makanisa Ulimwenguni, wanawaombea waamini ili waweze kuendeleza hija ya maisha na utume wao huko Pacific, kwa kutolea ushuhuda wwa upendo wa Mungu usiokuwa na kifani kwa waja wake. Kwa upande wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, hiki pia ni kiini cha furaha ya ushuhuda wa uwepo wa Roho Mtakatifu ulimwenguni. Huu ni mwaka ambamo Mabaraza ya Kiekumene Kikanda yanaadhimisha Mikutano yao mikuu.

Kanisa linawaombea wale watakaofanya mikutano yao Barani Afrika, Amerika ya Kusini na Ulaya. Baada ya Maadhimisho haya, Makanisa yote yatafanya hija ya maisha ya kiroho ili kwa pamoja waweze kushiriki Maadhimisho ya Mkutano mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwa mwaka 2013 utakaofanyika huko Busan, Korea ya Kusini, wakiongozwa na kauli mbiu ”Mungu wa maisha: tuongoze katika haki na ukweli”.

Marais wanawaalika waamini wanachama wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni kumfungulia nafsi zao Roho Mtakatifu ili waweze kimarishwa katika utekelezaji wa kufanya kazi pamoja kwa ajili ya haki ulimwenguni; haki ambayo ni njema; kwa kuendelea kutunza kazi ya uumbaji pamoja na kuleta amani pale ambapo kuna magomvi, chuki, misigano na vita.

Pentekoste iwe ni fursa kwa waamini kusali kwa ajili ya kuombea amani ambayo inahitajika sana ulimwenguni. Wanaombea ili Roho Mtakatifu aweze kuleta mabadiliko katika mioyo ya wote watakaohudhuria mkutano mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni utakaofanyika huko Busan, Korea ya Kusini.








All the contents on this site are copyrighted ©.